24.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

‘Atakayeruhusu CCM kushinda bila kupingwa kushughulikiwa’

Freeman Mbowe
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe

NA ELIZABETH HOMBO, DAR ES SALAAM

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe amesema kiongozi yeyote ndani ya chama hicho ambaye ataruhusu mgombea kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) kushinda uchaguzi bila kupingwa atashughulikiwa.

Mbowe alitoa kauli hiyo jana wakati akifungua uchaguzi wa Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA) uliofanyika katika ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Alisema katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na chaguzi nyingine zinazokuja, wakibaini kiongozi wa ngazi yoyote ndani ya chama hicho kuruhusu mgombea wa CCM kupitishwa kwa kigezo cha kupita bila kupingwa watamshughulikia.

“Hatutakubali kabisa kiongozi yeyote ndani ya chama kuruhusu mgombea wa CCM eti kwa sababu tu amepita bila kupingwa, tutamshughulikia.

“Pia wale ambao ni vibaraka ndani ya chama chetu, waendeleze ndoa zao na chama tawala cha CCM,” alisema Mbowe.

Akizungumzia uchaguzi wa BAVICHA, Mbowe aliwataka viongozi ambao watachaguliwa kuendeleza yale mazuri ambayo yalifanywa na viongozi waliomaliza muda wao.

Aidha Mbowe alisema endapo watabaini kiongozi yeyote ambaye hataruhusu chama kikue katika eneo lake, watamng’oa katika nafasi yake kwa kutumia Katiba yao ibara ya 6.3.4 inayoelezea kukoma kwa uongozi.

Mbowe aliwataka vijana hao baada ya kumaliza uchaguzi huo, wazungumze na kutoka na azimio la namna ya kuwandaa vijana na wazee ili waweze kujiandikisha katika daftari la wapigakura.

Awali akimkaribisha Mbowe, Mwenyekiti wa BAVICHA anayemaliza muda wake, John Heche, aliwataka vijana hao baada ya uchaguzi huo kuvunja makundi yote yaliyokuwapo wakati wanafanya kampeni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles