Allan Vicent – Tabora
JESHI la Polisi Mkoani Tabora, linamshikilia Omari Kabwindeke Nkuyu kwa tuhuma za kumuua mkewe Hawa Juma Seif (35) kwa kumchoma mkuki mgongoni na kutokezea upande wa pili kwenye ziwa la kushoto.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari jana, Kamanda wa Polisi mkoani hapa, ACP Barnabas Mwakalukwa, alisema tukio hilo lilitokea Februari 24 saa 2.00 usiku katika Kitongoji cha Barabara ya Nzega, Kijiji cha Isikizya wilayani Uyui.
Alibainisha kuwa mtuhumiwa huyo alimvizia marehemu (mkewe) akiwa amelala usiku na kumchoma mkuki mgongoni ambapo ulitokezea upande wa pili kwenye ziwa la kushoto.
Alisema uchunguzi wa awali unaonesha chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa kimapenzi baina ya wawili hao huku akibainisha kuwa matukio mengi ya mauaji katika mkoa huo yamekuwa yakichochewa na ugomvi wa mali, mashamba, wivu wa kimapenzi na kulipiza kisasa.
Kamanda Mwakalukwa alisema upelelezi wa shauri hilo unaendelea na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani utakapokamilika.
Alitoa wito kwa jamii kubadilika na kuacha kuchukua sheria mkononi hali inayopelekea mauaji ya watu wasio na hatia, aliwataka kutumia njia zinazofaa ikiwemo vyombo vya kisheria ili kufikia mwafaka wa matatizo au migongano yao.