27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Albino wazichapa kavukavu Ikulu

Na Asifiwe George, Dar es Salaam
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino), wamepigana ngumi na mateke wakigombea kuingia kumwona Rais Jakaya Kikwete, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Tukio hilo la aina yake lilitokea jana majira ya saa nne asubuhi ambapo lilianzia kwenye eneo la mapokezi Ikulu mara baada ya walemavu hao kukaguliwa na kuwekwa kwenye chumba maalumu cha kupumzikia wageni.
Baada ya muda, ofisa wa Ikulu alifika kwenye chumba walipokuwa walemavu hao akiwa na karatasi yenye orodha ya watu 15, ambao ndiyo waliopaswa kumwona Rais.
Baada ya ofisa huyo kuanza kusoma majina ya wahusika, albino wote waliokuwa kwenye chumba hicho walinyanyuka kutoka kwenye viti vyao na kusimama karibu na mlango, ambako alikuwa amesimama.
Kila ofisa huyo alipokuwa akisoma jina, mhusika alitoka nje ya chumba hicho tayari kwa kwenda kumwona Rais.
Baada ya ofisa huyo kumaliza kusoma majina hayo, alisema: “Hawa ndio wanaokwenda kuwawakilisha kwa sababu hamuwezi kuingia kundi lote hili.”

VURUGU
Baada ya majina hayo kutajwa, mmoja wa albino hao, Nuru Chagutu, ambaye hakutajwa, alisema hakubalini na kitendo cha viongozi pekee kumwona Rais ili hali wajumbe wengine ambao pia ni wahathirika wa mauaji ya albino wakibaki getini.
Alisema pia yeye na wanaharakati wenzake wa Chama cha Tunataka Haki ya Kuishi (THK), hawamtambui Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu wa Ngozi Tanzania (TAS), Ernest Kimaya, ambaye alikuwa kwenye orodha ya watu 15 waliopangwa kumwona rais.
Alihoji pia sababu za Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Walemavu Tanzania (Shivyawata), Amon Mpanju, ambaye si mlemavu wa ngozi, kuwamo kwenye orodha hiyo huku akiwa si mlemavu wa ngozi.
“Kama huyu mtu mweusi (Mpanju) ataingia pamoja na mwenyekiti (Kimaya) na sisi tutaingia, vinginevyo mkutano ufe,” alisema Nuru.
Baada ya maelezo hayo, watu waliokuwa wamechaguliwa nao walionekana kutoridhishwa na kauli ya Nuru, hivyo kukaibuka kurushiana maneno kati ya pande hizo mbili.
“Kama sisi hatuingii, chukueni simu zenu tutoke wote, hakuna kubaki mtu ndani, wote tuondoke, mkutano umekufa,” alisikika mtu mwingine akisema.
Baada ya kurushiana maneno kuzidi, ofisa mmoja na Ikulu aliamuru walemavu hao pamoja na waandishi wa habari waliokuwa kwenye eneo hilo watoke nje.
Baada ya amri hiyo, watu wote walitoka nje ya chumba hicho cha mapokezi na kuendelea kurushiana maneno wakiwa kwenye viwanja hivyo vya Ikulu.
Ofisa huyo wa Ikulu aliwafuata tena na kuwaambia: “Ninaposema mtoke nje, ninamaanisha ni nje ya geti.”
Baada ya kauli hiyo, wale waliokuwa wametajwa majina tayari kwenda kumwona Rais, walirudi tena kwenye chumba cha mapokezi kuchukua simu zao tayari kwa kutoka nje ya geti.
“Chukueni simu tuondoke, hakuna kubaki mtu, leo hakuna kusaini (kuchukua fedha),” alisikika mmoja wa walemavu hao akisema.

NJE YA GETI
Baada ya kutoka nje ya geti la Ikulu, waliendelea kumwandama Kimaya kwamba hawamtambui na kuwa hata ofisi alizokuwa akizitumia kwa sasa zimefungwa.
“Yanapotokea matukio ya mauaji tunapowaambia viongozi wetu atumwe hata mwakilishi, wamekuwa wakikataa huku wakisema ‘kufa, kufaana’, hiyo si sahihi, wao wananeemeka na kuota vitambi na kupewa magari, lakini sisi tumekuwa tukiendelea kuteseka,” alisema Nuru.
Baada ya kauli hiyo, Kimaya alimpiga teke Nuru huku akimwambia; “huwezi kutunyima haki ya kuingia kwenye kikao kumsikiliza Rais.”
Baada ya Kimaya kumpiga Nuru, walemavu wengine waliokuwa wakimpinga mwenyekiti huyo wa TAS, walianza kumshambulia kwa maneno.
“Kwanini unampiga Nuru wakati anakwambia ukweli? Kwanza muda wako ulishakwisha. TAS hakuna viongozi na ofisi zimefungwa…hatukubali, tunakupiga na kwenye kikao tunaingia wote?” alisikika mmoja wa walemavu hao aliyetambulika kwa jina la Amon Anastaz.
Baada ya vurugu hizo kuendelea kwa dakika kadhaa, ofisa wa Ikulu aliyekuwa na beji kifuani yenye jina la Andrew M.M.S, aliwataka walemavu hao kupanda magari waliyokuja nayo na wakachaguane ili wapate wawakilishi wanaowataka.
Walemavu hao kwa ujumla wao walitii amri hiyo na kuondoka.

POSSI AWASIKITIKIA
Dk. Abdallah Possi, mtaalamu wa sheria ambaye alikuwa miongoni mwa walemavu wa ngozi ambao walikuwa waingie kwenye kikao hicho, alisema kitendo kilichofanywa na wenzake hao ni cha aibu.
Alisema kitendo hicho si njia ya kupata suluhisho la matatizo yanayowakabili watu wa jamii hiyo.
“Tukio la leo ni aibu sana, jamii haiwezi kutuelewa kwa sababu tunagombana wenyewe kwa wenyewe badala ya kukaa na kuangalia namna ambavyo tunaweza kusaidiwa, badala yake tumeanza kutupiana maneno na kupigana.
“Kinachotakiwa sasa ni kukaa pamoja na kuelewana kwani sisi wote ni kitu kimoja, tunahitaji msaada wa jamii yote, tuna haki ya kuishi kwa amani bila kubaguliwa au kuuliwa katika nchi yetu,” alisema.
Alibainisha kuwa kiini cha vurugu hizo hakijui zaidi ya kuona ngumi, jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa kuna tatizo ndani ya chama chao.
Alisema kutokana na hali hiyo, wameiomba Serikali kuwasaidia ili kuondoa mgogoro ndani ya chama hicho ambao unaweza kuongeza matatizo badala ya kuyatatua.
Baada ya tukio hilo, ambalo lilidumu kwa takribani dakika 30, waliokuwa wameteuliwa kuongea na rais, walipata fursa hiyo baada ya wale waliokuwa wakileta vurugu kuondoka eneo hilo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles