Walter Mguluchuma – Katavi
MKAZI wa Mtaa wa Hoteli Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi, Medadi Basiliyo, amenusulika kifo baada ya kupigwa na wananchi baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kuiba jeneza la chuma linalotumiwa na waumini wa Kanisa Katoliki kubebea maiti za watoto kwenda kuzikwa ambalo alitaka kuliuza kwa bei ya Sh 8,000.
Akizungumza jana baada ya mtuhumiwa huyo kukamatwa katika sakata hilo, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mpanda Hotel, Christina Ibrahimu, alisema tukio hilo lilitokea jana saa tabo asubuhi na kuvuta hisia za wananchi.
Alisema mtuhumiwa huyo ni mlinzi kwenye maeneo ya watu binafsi alikuwa akiishi katika nyumba ya Mwenyekiti wa Mwenyekiti wa Kigango cha Mpanda Hoteli kama mpangaji ambapo ndipo jeneza hilo huifadhiwa katika nyumba hiyo.
Alisema jeneza hilo hutumiwa na waumini kwa kuwa wengine huwa hawana uwezo wa kutengeneza sanduku la kuzikia na hulazimika kutimia kwa ajili ya shughuli hiyo.
“Baada ya kuibiwa kwa jeneza hili taarifa ilikuja kuripotiwa katika ofisi ya mtaa mbapo zilianza jitihada za kulitafuta kwa ushirikiano na wananchi na viongozi wa mtaa.
“Wakati msako ukiendelea waliona mtu amebeba jeneza hilo ambapo mmoja wa wananchi hao Libelatus Nzelani alisema kuwa amemuona mtu amebeba jeneza la maiti na alisema baada ya kumuuliza anapeleka wapi ndipo mtuhumiwa huyo alipomjibu kuwa kama analihitaji basi yuko tayari kumuuzia.
“Ndipo alipomtaka amtajie bei na alimwambia ampatie Shilingi 8,000 tu, ndiyo aweze kumuuzia jeneza hilo jambo lilomfanya aingiwe na shaka kwamba na kuanza kupiga mayowe ya wizi na watu walifika na kuanza kumdhibiti,” alisema Ibrahim
Alisema baada ya wananchi hao kufika walianza kumpiuga mtuhumiwa huyo jambo ambalo lilimfanya wahi kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ambao walifika haraka na kumnusuru mtuhumiwa huyo na kichapo.