31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Sakata uuzwaji Cocobeach lageuka

Pg 4Na Jonas Mushi, Dar es Salaam

WAKATI  Serikali ikimsimamisha kazi aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Mhandisi Mussa Natty, kwa madai kuwa pamoja na mambo mengine alihusika kuuza ufukwe wa Cocobeach, sakata hilo limevaa sura mpya baada ya Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea na Diwani wa Kata ya Ubungo, Boniface Jacob, kuibuka na kutoa mktaba unaaonyesha kuwa eneo hilo liliuzwa kabla ya Mhandisi huyo kuanza kazi Kinondoni.

Mbunge huyo na Diwani ambao wote wanatoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), jana waliwaeleza waandishi wa habari kuwa, Natty kawajibishwa kwa sababu za kisiasa ikiwemo kutenda haki katika Uchaguzi Mkuu uliopita.

Katika uchaguzi huo, majimbo ya Wilaya ya Kinondoni yote yalichukuliwa na vyama vinaunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), jambo ambalo viongozi hao walisema Natty alitakiwa kutangaza washindi kuwa ni wagombea wa CCM.

Akielezea suala hilo, Diwani wa Ubungo,  Boniface Jacob,  alisema tangu kumalizika kwa uchaguzi wameshuhudia wakurugenzi mbalimbali wa halmashauri ambazo wapinzani wameshinda wakishughulikiwa kwa mgongo wa kutumbua majipu.

“Nafsi zetu zinatusuta endapo tukikaa kimya huku tunaona wakurugenzi wa halmashauri wanashughulikiwa kwasababu walikataa kutekeleza maagizo haramu kipindi cha uchaguzi   ikiwemo Kinondoni na wengine wa Mbeya, Iringa na Mtwara.

“Kama kuna ufisadi umetokea hatutamtetea mtu na kama kuna mtu tunaona anaonewa hatutakaa kimya na hili la Natty tunamwomba Rais John Magufuli aunde tume huru ambayo haitahusisha TAMISEMI wala Wizara ya Ardhi akiwemo Lukuvi (Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi), kwa sababu wana masilahi katika suala hilo,” alisema Jacob.

Alisema anashangazwa na tuhuma zilizotangazwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Jumanne Sagini ya kumsimamisha kazi Natty.

Katika tangazo lake, SSagini alidai kuwa Natty anatuhumiwa kwa usimamizi mbaya wa ujenzi wa barabara, ukosefu wa uadilifu katika ubinafsishaji wa ufukwe wa Coco na malalamiko ya wananchi juu ya viwanja katika eneo la Kinondoni.

“Ukiangalia suala la barabara kitabu cha makabidhiano ya halamashauri cha mwaka 2010 kinaonesha mikataba yote ya barabara hizo,  Natty aliingia kazini akaikuta mikataba ya barabara imekwishasainiwa na wakurugenzi waliomtangulia akiwemo Ndunguru (Raphael Ndunguru 2009-2011) na Fwema (Fortinatus Fwema 2011-2013).

“Ndunguru ndiye aliyeleta miradi ya lami nyepesi ambazo zinagharimu milioni 500 kwa kilometa moja baada ya kutoa hoja kuwa barabara za vumbi zinagharimu milioni 300 na mvua zikinyesha zinaharibika upesi hivyo bora ziwekwe lami nyepesi na ziwe zinafanyiwa ukarabati pale zinapoharibika.

“Hapo Natty anahusika vipi ikiwa waliomtangulia ndio walioidhinisha kiwango cha barabara na walijua lazima ziwe zinaharibika baada ya muda fulani,” alisema Jacob.

Kuhusu tuhuma ya malalamiko ya wananchi kuhusu viwanja alisema migogoro ya ardhi ilikuwepo tangu zamani na imeendelea kuwepo nchi nzima, hivyo madai hayo hayana mashiko.

Mkataba wa uuzwaji wa fukwe

Kwa upande wake Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea, alieleza namna ubinafsishwaji wa Coco beach ulivyofanyika ambapo alimtetea Natty na kusema kuwa mchakato wa kuuzwa kwa ufukwe huo ulianza muda mrefu kabla ya mkurugenzi huyo kushika wadhifa huo.

Kubenea alionesha mkataba wa makubaliano kati ya Baraza la Manispaa ya Kinondoni na Q- Consult Limited kampuni inayomilikiwa na mfanyabiashara Yusuph Manji ambaye ndiye mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo.

Mktaba huo ulisainiwa Desemba 21, mwaka  2007 ambapo kwa upande wa Manispaa ya Kinondoni ulisainiwa na Naibu Meya wa wakati huo, Julian Bujugo na Mkurugenzi wa Manispaa ambaye alikuwa ni Noel Mahyenga huku upande wa Q-Consult ukisainiwa na S. Sampatihkumar na B. N. Arvind wote wakiwa wakurugenzi katika kampuni hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles