25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Sheikh Ponda: Nitaendelea kupambana

Pg 1Na Ramadhan Libenanga, Morogoro

KATIBU wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, ameachiwa huru baada ya kukaa mahabusu kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili.

Hata hivyo baada ya kuachiwa huru na Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro, Sheikh Ponda amesema licha ya kuachiwa ataendelea kupambana kupigania haki za Waislamu nchini.

Katika mazungumzo yake, Sheikh Ponda alisema amesikitishwa na kitendo cha Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kuchelewesha haki yake ya kuwa huru.

Akizungumza jana baada ya kuachiwa huru na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Morogoro, Marry Moyo, Sheikh Ponda alisema kukaa kwake  ndani  kwa  miaka miwili na miezi mitatu kunamfanya  kuona umuhimu wa  mabadiliko  ya Katiba iliyokuwa  ikidaiwa na wananchi.

Alisema Katiba mpya inayohitajika ni ile  ambayo  ingeweza  kupoka   baadhi  ya madaraka   katika  vyombo  vya  sheria  na  dola  kama  ilivyokuwa  katika kesi  yake ambapo  dhamana  yake  ilizuiliwa na mtu mmoja tu bila sababu za msingi.

“Nimefurahi  kupata  haki  yangu  lakini  bado nalalamikia  haki  yangu  ya  dhamana  ilizuiliwa na  Mkurugenzi wa Mashtaka  bila  sababu, huku  wakijua  kuwa sina  kosa la kujibu.

“Kukaa kwangu ndani kwa  kipindi cha miaka  miwili na miezi  mitatu kumenifanya kuona  umuhimu wa  mabadiliko  ya Katiba  iliyokuwa  ikilalamikiwa na  Watanzania. Hili tutaendelea kupambana nalo dhamana ni haki yangu lakini ilizuiliwa na mtu mmoja tu,” alisema Sheikh Ponda.

Awali Mahakama ya  Hakimu  Mkazi  Mkoa wa Morogoro  ilimwachia  huru  Sheikh Ponda, ambaye alikuwa akikabiliwa na tuhuma za uchochezi.

Akisoma  hukumu  hiyo jana, Hakimu Moyo alisema  kuwa  mahakama  imejiridhisha  baada ya kupitia  vielelezo  na mwenendo wa kesi  iliyokuwa  ikimkabili  na  kuona  kuwa mtuhumiwa  hana hatia, hivyo akaamuru aachiwe  huru .

Mara baada ya maelezo hayo, Hakimu Moyo alisema kuwa kutokana na kifungu 235 kifungu kidogo cha (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 mahakama inaona mshtakiwa huyo hana kosa,  hivyo inamwchia huru.

Hakimu Moyo alisema katika kesi hiyo, Jamhuri ilikuwa na mashahidi tisa pamoja na vielelezo saba, huku upande wa utetezi ukiwa na shahidi mmoja ambae alionekana kupingwa na upande wa Jamhuri kwa madai kuwa amekuwa akifuatilia mwenendo wa kesi.

Sheikh Ponda alikuwa akituhumiwa kutamka maneno ambayo yalionekana kuumiza dini nyingine (maneno ya kichochezi) na kufanya mkutano usio halali Agosti 8, 2013 maeneo ya Kiwanja cha Ndege mkoani hapa.

Mahakama hiyo iliweza kumfutia mshtakiwa shtaka namba moja la kukiuka masharti ya Mahakama ya Kisutu ya jijini Dar es Salaam kwa kuwa mtuhumiwa alikata rufaa na kuweza kushinda rufaa yake hiyo.

Baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi ya mkoani hapa kufuta shtaka namba moja, mshtakiwa alibakiwa na mastaka mawili ambayo alitakiwa kuyajibu na mara baada ya mahakama hiyo kupitia maelezo ya pande zote imeona mshtakiwa hana hatia.

Sheikh Katimba

Msemaji wa Jumuiya na Taasisi za  Kiislamu Tanzania, Sheikh Rajab Katimba  alisema  Waislam nchini  kote wamefurahia  kutendeka  kwa  haki , japo  haki  hiyo  ilicheleweshwa.

Alisema  kuwa kesi  ya Sheikh Ponda   haikuwa  na itikadi za kidini  wala  siasa  ndio  maana  hata  wanasheria  wake  walikuwa  kutoka  katika   imani  tofauti , hivyo amesema  kuwa lengo  lilikuwa kutafuta  haki za kiimani.

“Wanachotaka  Watanzania  ni  kuona  keki ya  nchi  inaliwa  na  Watanzania  wote  bila  kujali  itikadi za kidini wala  siasa,” alisema Katimba.

Sheikh Katimba awewataka wafuasi wa Ponda pamoja na waumini wa dini hiyo kuwa watulivu, kwa kuwa kiongozi wao ameshinda kesi yake ambapo walisema watakaa wote kwa pamoja ili kujua nini kiongozi wao anatakiwa kukifanya kwa sasa.

Wakili wake anena

Miongoni mwa mawakili watatu waliokuwa wakimtetea Sheikh Ponda ni Abubakar Salim, ambaye alisema anafurahishwa na maamuzi hayo, kwani mahakama imetenda haki japokuwa haki hiyo imecheleweshwa.

Alisema kama Serikali haitakubaliana na maamzi hayo na kuamua kukata rufaa wao wako tayari.

Salim alisema kwamba, watakaa na mteja wao ili kuona kama anahitaji kufungua kesi kuishtaki Serikali kwa kumpotezea muda, ikiwa ni pamoja na kumnyima dhamana waweze kuifungua ila kama atawasamehe hayo ni maamuzi yake mwenyewe.

“Tunashukuru mteja wetu ameshinda kesi ambayo naiona kama ilikuwa ya kutengenezwa na watu kwa manufaa yao. Waswahili walisema mwisho wa ubaya ni aibu sasa kama Ponda atafungua kesi ya madai sisi tupo tayari,”alisema.

Sheikh Ponda alizaliwa miaka 56 iliyopita alikamatwa  Agosti 19, 2013 na kushtakiwa kwa makosa matatu na baadaye kufutiwa kosa namba moja na kubaki na mashtaka mawili.

Ponda alinyimwa dhamana kwa kile kilichodaiwa ni sababu za kiusalama kulingana na kosa lake. Ponda amekaa mahabusu kwa miaka miwili na miezi mitatu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles