31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Kingunge: Mabadiliko lazima

kingunfNA FREDY AZZAH, ARUSHA

MWANASIASA mkongwe nchini, Kingunge Ngombale Mwiru, jana kwa mara ya kwanza alipanda jukwaani kumnadi mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa na kusema mabadiliko ni lazima.

Kingunge aliyasema hayo jijini Arusha kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika viwanja vya Shule ya Msingi Sinoni.

Kingunge alihutubia huku mvua ikinyesha, lakini wananchi waliokuwa eneo hilo hawakuondoka.

“Historia yangu, nimeshiriki katika kuleta mabadiliko na ninaamini kwa dhati ya moyo wangu kwamba kwa sasa mabadiliko katika Tanzania ni lazima, sisi tumekuwa huru kwa miaka 54 sasa.

“Tulivyounda Tanu tulitaka chombo cha mabadiliko na Zanzibar  walivyounda Afro Shirazi walitaka kuwakomboa Waafrika wenzao, vyama vyote viwili vilitaka Watanzania tupate mabadiliko na baadaye kwakuwa waliamini katika mabadiliko, waliunganisha vyama na baadaye nchi, na mimi nilikuwa kwenye kamati ya watu 20 kuanzisha CCM.

“CCM katika miaka ya karibuni kimekuwa na dalili zote kwamba baada ya kuwa madarakani kwa nusu karne kimeishiwa pumzi,” alisema Kingunge na kushangiliwa.

Ili kutuliza watu hao, mkongwe huyo wa siasa kwa mara ya kwanza alilazimika kutumia salamu maarufu ya Chadema ya “peoples” hatua iliyofanya umati huo ulipuke zaidi kwa shangwe na kelele na kujibu “power”.

Kingunge alisema maendeleo ya watu ni sawa na kupanda mlima, hivyo kuhitaji pumzi ya kutosha jambo ambalo CCM hawana.

“Lazima uwe na pumzi kila unapozidi kwenda mbele, ni wale tu wenye pumzi ndio watafika kileleni, CCM sasa pumzi imekwisha.

“Tanzania imefikia asilimia 7, Rais Kikwete alipokea nchi wakati uchumi ukiwa na asilimia 7, miaka 10 baadaye kwa taarifa za Serikali uchumi unakua kwa kasi ndogo sana, kidogo, chini ya asilimia 7, maana yake uchumi umeganda huku wenye mahitaji wakizidi kuongezeka, hivyo tunahitaji mabadiliko.

“Lazima ipatikane timu nyingine ya Watanzania hawa hawa, na timu hiyo ipo, wakabidhiwe dola wachochee mabadiliko ili kupambana na umasikini, lazima mfumo wa uchumi ukue kwa zaidi ya asilimia 10, CCM kwa miaka 10 wamebaki kwenye asilimia 7.

“Kwahiyo nasema wapo watu Tanzania wanaoweza kutupeleka mbele hata ya asilimia 10, lazima tumpate kiongozi atakayeweza kutupeleka mbele, kiongozi huyo yupo, nyie mnamjua,” alisema na kuhoji “Ni nani?”  wananchi wakajibu “Lowassa”.  Akasema “Semeni tena”, wakajibu tena “Lowassa”.

“Ndiyo maana mimi nipo hapa, na nilikuwapo siku ile Lowassa alipotangaza nia, nilikuwa naye sambamba, mimi ninaamini ana sifa za kutuondoa hapa, mtu hawezi kufanya miujiza ya kutuondoa hapa kama hana watu.

“Ndiyo maana nilisema pale, sifa ya kwanza kubwa ni je, ana watu nyuma yake? Na Baba wa Taifa alituambia, ‘mnapotafuta kiongozi wa nchi msikae kwenye vikao vyenu mkaamua, sikilizeni watu wanasema nini’.

“Hayo ni maoni ya Watanzania na ndiyo maoni yangu. Na huu (umati uliokuwa uwanjani hapo) ni ushahidi kwamba ana watu nyuma yake, Mwalimu alisema katika mazingira ya vyama vingi tupingane bila kupigana, ni wananchi, sasa tunaenda kwenye uchaguzi tarehe 25 kufanya maamuzi na wanaofanya maamuzi ni wananchi wa Tanzania.

“Ikulu ni kura siyo maneno, mazungumzo ya uwanjani hayatupi rais, kura zinatupa rais, kwahiyo tudhamirie tarehe 25 Oktoba twende kwenye vituo vya uchaguzi, kazi yetu iwe moja tu, msikubali kubabaishwa, kazi yenyewe ni kila mmoja ukifika pale, unachukua, unaweka Lowassa.

“Nawaomba sana, rafiki zangu wa CCM nimekuwa nao, wasibabaike, uamuzi wa kuchagua anayefaa unao wewe, na ninyi ndugu zangu niliowaacha CCM sikuwaacha kwa sababu nawachukia, mimi napenda Watanzania wote, nimeondoka kwa sababu sikubaliani na uongozi unaovunja katiba ya chama, taratibu za chama,” alisema.

Kingunge ambaye alipanda jukwaani saa 10:53 jioni na kushuka saa 11:27, alisema amekuwa akifuatilia mikutano ya kampeni ya vyama vyote na amefurahishwa na Ukawa kuendesha kampeni zao kistarabu bila kumtukana mtu.

“Chadema na Ukawa mmetia fora, ninyi mmeonyesha ustaarabu, utulivu na heshima kwa nchi yetu, hata watazamaji wameliona hilo, pamoja na kwamba mikutano yenu inakutanisha maelfu ya watu, kuna utulivu na adabu, kwa bahati mbaya chama ambacho mimi kilikuwa chama changu, tangu waanze kampeni wamefanya maajabu na vituko.

“Wameanza na matusi ya kustaajabisha, na kwa bahati mbaya pamoja na kwamba CCM ina sera nyingi tu, hawazungumzii sera, wanazungumza mtu, watu wazima waliokuwa wamepumzika wamewachukua kuja kwenye majukwaa kumzungumzia mtu, kwahiyo ni lazima mtu anayezungumzwa sana awe mtu mzito sana,” alisema.

 

WATU WAZIMIA

Licha ya kwamba uwanja huo ulikuwa ni mkubwa, takribani watu 50 walipoteza fahamu kutokana na kukosa hewa kulikosababishwa na msongamano kuwa mkubwa.

 

LOWASSA

Akihutubia wananchi hao, Lowassa aambaye anaungwa mkono na vyama vya CUF, NLD na NCCR-Mageuzi, alimshukuru Mzee Kingunge kwa kumuunga mkono huku akimtaja kwamba ni kati ya nguzo za Tanu na CCM.

“Nimefanya kazi kwa miaka mingi na Kingunge, ndiye alikuwa nguzo ya CCM na Tanu, kwahiyo watakuwa wamepata pigo sana,” alisema.

Kuhusu sera zake endapo ataingia madarakani, alisema  atakabiliana na matatizo mbalimbali ya Watanzania, ikiwamo sekta ya afya kwa kuhakikisha kila wilaya inakuwa na hospitali ya rufaa.

 

SUMAYE

Naye Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, jana alikumbushia ukaguzi uliofanywa na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa mwaka wa fedha 2014/15 ambao umeibua ufisadi mkubwa katika wizara, idara, wakala za Serikali, halmashauri, taasisi na mashirika ya umma.

Alisema anashangazwa na Wizara ya Ujenzi inayoongozwa na mgombea wa CCM, John Magufuli kubainika kufanya malipo hewa ya Sh milioni 951.7 na kupoteza Sh bilioni 124.8 ambazo ni malimbikizo ya riba kutokana na kuchelewesha malipo ya wakandarasi.

“Mimi nashangaa huu uadilifu wanaosema, gazeti la MTANZANIA juzi limechapisha ripoti inasema Wizara ya Magufuli imesababisha upotevu wa Sh bilioni 125, huu ni ufisadi mkubwa,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles