28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Chadema wajadili mgombea urais

NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
KAMATI Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imekutana jijini Dar es Salaam ambapo itajadili masuala mbalimbali ikiwemo suala la mgombea urais kupitia vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Mbali na ajenda hiyo pia Kamati Kuu itajadili hatima ya uchaguzi mkuu pamoja na uandikishaji wa daftari la wapiga kura kupitia mfumo wa BVR.
Ukawa ni umoja ulioanzishwa Februari mwaka jana ukiwa ni kikundi shinikizi katika mchakato wa Katiba unaoundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD.
Mmoja wa viongozi wa juu wa Chadema aliimbia MTANZANIA kuwa katika kikao hicho cha Kamati Kuu kilichoanza jana pamoja na mambo mengine suala la mgombea urais kupitia Ukawa liliwasilishwa ikiwa ni moja ya azimio la Ukawa la kutaka kila chama kijadili suala hilo katika vikao vyake vya maamuzi.
Hatua hiyo ya Chadema inatanguliwa na ile ya Chama cha Wananchi (CUF), ambacho kilifanya kikao chake wiki mbili zilizopita ambapo pamoja na mambo mengine kilitoa taarifa za kuridhishwa na mwenendo wa kupata mgombea mmoja wa kila ngazi ya urais, ubunge na udiwani kupitia Ukawa.
MTANZANIA lilipomtafuta Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salumu Mwalimu alisema pamoja na mambo mengine lakini kikao hicho kitajadili hali ya uandikishaji wapiga kura kwa mfumo wa BVR.
“Kikao hiki cha Kamati Kuu kitajadili kwa kina ajenda ya taarifa ya hali ya kisiasa nchini, mfumo wa uandikishaji wa kielekroniki (BVR), mkakati wa ushiriki na ushindi wa Uchaguzi Mkuu,” alisema Mwalimu.
Mbowe ahofia uchaguzi
Awali akifungua kikao cha Kamati Kuu, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alisema kuna dalili za kuahirishwa kwa Uchaguzi Mkuu hali inayochangiwa na kusuasua kwa uandikishaji wapiga kuwa.
Alisema kutokana na hali hiyo hadi sasa Rais Jakaya Kikwete, hana uhakika wa kuwepo Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
“Pamoja na kwamba Rais Kikwete amesema kuwa Uchaguzi Mkuu upo palepale pamoja na kura ya maoni ambayo najua kabisa bado Bunge halijakaa kufanya mabadiliko ya sheria ili kuruhusu kuendelea.
“Hadi sasa hakuna mazingira yanayoonyesha kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu zaidi ya kusikika kwa maneno yasiyoendana na vitendo,” alisema Mbowe.
Kuporomoka shilingi
Mwenyekiti huyo wa Chadema, alisema kutokana na kutotabirika kwa kuwepo Uchaguzi Mkuu kwa vitendo kumechangia kwa kisiasi kikubwa kuporomoka kwa shilingi ya Tanzania jambo ambalo ni hatari kwa uchumi wa nchi.
“Usalama, uchumi na uwekezaji umeyumba hali hiyo imechangia kuyumba kwa sarafu na anayestahili kupewa lawama hizo ni Rais Kikwete kwani hana uhakika wa uchaguzi, hivyo hata waziri mkuu hawezi kuwa na uhakika wake.
“Mwekezaji anataka kuona uhakika wa uwekezaji wake hivyo wanahitaji kuwekeza katika nchi inayotabirika, hivi sasa wawekezaji wamesimamisha miradi yao kutokana na kutojua hatma yao hali iliyosababisha kushuka kwa zaidi ya Shilingi 400,” alisema Mbowe.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa pamoja na kushuka kwa shilingi lakini anashangaa kuwaona viongozi nchini wakichukulia hali hiyo kama ya kawaida.
“CC ya Chadema pamoja na mambo mengine itajadili mustakabali wa uchaguzi mkuu hasa, kutafuta ufumbuzi wa suala hilo ambapo tutatoka na uamuzi wa nini kifanyike,” alisema Mbowe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles