27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bango la walimu lazua gumzo Mei Mosi

Na Elizabeth Mjatta
BANGO lililobebwa na walimu katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi jana likiwa na maandishi yanayosomeka “Shemeji unatuachaje?”, limezua gumzo katika maeneo mbalimbali nchini, hususan katika mitandao ya kijamii.
Jana katika maadhimisho hayo ambayo kitaifa yalifanyika mkoani Mwanza na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali, walimu walipita mbele ya Rais Kikwete ambaye alikuwa mgeni rasmi huku wakiwa wamebeba bango hilo.
Wakipita mbele ya Rais Jakaya Kikwete, walimu hao walilielekeza bango hilo upande wake ili aweze kulisoma vizuri.
Picha zilizochukuliwa za walimu hao wakiwa wamebeba bango hilo, zilisambaa kwa kasi jana hiyo hiyo kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii, hususani ule wa WhatsApp.
Walimu wamekuwa wakimuita Rais Kikwete shemeji kutokana na mke wake, Mama Salma, kutoka katika kada hiyo.
Mama Salma Kikwete kabla ya mume wake hajawa Rais alikuwa ni mwalimu wa shule ya msingi, akiwa amefundisha shule kadhaa, ikiwemo ya Mbuyuni, jijini Dar es Salaam.
Mara nyingi walimu kupitia Chama cha Walimu Tanzania (CWT), wamekuwa katika mgogoro na Serikali kutokana na kudai malimbikizo ya madeni yao.
Chama hicho, ambacho kinaongoza walimu wa shule za msingi na sekondari wapatao 206,000 kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2010, kimekuwa pia miongoni mwa vyama vinavyopinga mchakato wa Katiba mpya.
Bango hilo jana limeibua mjadala mkali, huku wengine wakiwapongeza walimu kwa ubunifu wao, wengine wakisema Kikwete atawaacha kama alivyowakuta.
Tofauti na mtazamo wa wengi, hata hivyo, Rais Kikwete alisema anaondoka madarakani akiwa amefanikiwa kuboresha mishahara ya wafanyakazi nchini, ikiwemo ya walimu.
Wakati anaingia madarakani mwaka 2005, kima cha chini cha mshahara kilikuwa Sh 65,000 na sasa kimefikia Sh 265,000.
Alisema katika bajeti ijayo kima cha chini kinaweza kikaongezeka na kufikia Sh 300,000.
Kwa utani Rais Kikwete alisema huku akicheka; “Shemeji zangu baada ya hayo nawapongeza kwa kufungua benki ya walimu…kuoa mwalimu ni tatizo”.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles