Na JANETH MUSHI -ARUSHA
MAWAKILI wanaomtetea Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema) katika kesi ya kuhamasisha watu kukusanyika na kufanya maandamano kinyume cha sheria, wameomba shauri hilo kuhamishiwa Mahakama Kuu mbele ya jopo la majaji watatu kutokana na kuwapo kwa masuala ya kikatiba kwenye hati ya mashtaka.
Lema anashikiliwa katika mahabusu ya Gereza Kuu la Kisongo kwa zaidi ya miezi miwili, baada ya kukosa dhamana ya kesi mbili (namba 440 na 441) za uchochezi dhidi ya Rais Dk. John Magufuli. Alikamatwa Novemba 2, mwaka jana.
Mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Benard Nganga, kesi hiyo namba 352 ya mwaka jana, ilitarajiwa kuanza kusikilizwa jana kwa shahidi wa kwanza, Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Arusha (RCO), George Katabazi kutoa ushahidi wake ambao ulikwama, baada ya wakili wa utetezi kudai kuwa na hoja za kisheria.
Katika kesi hiyo ambayo Lema anadaiwa kuhamasisha maandamano ya Ukuta yaliyopangwa kufanyika Septemba mosi, mwaka jana, upande wa Lema unawakilishwa na mawakili John Mallya na Sheck Mfinanga, huku Jamhuri ikiwakilishwa na Wakili Alice Mtenga.
Wakili Mallya, alidai kuwa masuala ya kikatiba ambayo yamehusishwa kwenye hati ya mashtaka katika mahakama hiyo ya chini mashahidi wa upande wa jamhuri hawataweza kujibu pale watakapokuwa wanahojiwa na mawakili wa utetezi.