25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

KIMBEMBE FAINALI SIMBA, AZAM KOMBE LA MAPINDUZI LEO

*Yanga yawashtua watani wao Simba


 

simba-vs-azamNA SAADA SALIM, UNGUJA

FAINALI ya Kombe la Mapinduzi inayozikutanisha timu za Simba na Azam, inatarajia kufanyika leo katika Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Hii ni mara ya pili kwa timu hizo kucheza fainali ambapo mwaka 2012 tarehe kama ya hii, zilikutana katika uwanja huo na Azam kuibuka mabingwa kwa mara ya kwanza katika michuano hiyo baada ya kuifunga Simba 2-1.

Simba imetinga fainali baada ya kuwasukuma nje ya michuano mahasimu wao Yanga, kwa mikwaju ya penalti 4-2, wakati Azam wao waliifunga Taifa Jang’ombe bao 1-0.

Katika mchezo huo, Simba itakuwa ikiongozwa na Mcameroon Joseph Omog, aliyewahi kukifundisha kikosi cha Azam misimu miwili iliyopita ambapo hakufanikiwa kutwaa kombe hilo na kuishia hatua ya nusu fainali.

Azam imeshiriki Mapinduzi ikiwa chini ya kocha msaidizi, Iddy Nassor `Cheche` ambaye amekaimu nafasi ya kocha mkuu baada ya uongozi wa timu hiyo kumuondoa kocha mkuu, Zeben Hernandez, lakini kocha huyo ameonekana kumudu mikiki mikiki na kuivusha timu katika fainali.

Mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu, kwani makocha wa timu hizo Omog na Cheche wanatumia mfumo wa kujaza viungo.

Akizungumzia mchezo huo, Omog alisema anaifahamu vizuri Azam kutokana na baadhi ya wachezaji wengi walikuwepo katika kikosi hicho kuwafundisha.

“Azam wanatumia mfumo wa kuchezesha viungo kama mimi, lakini kwa upande wangu sitaweka silaha zangu hadharani, naweza kufanya lolote uwanjani.

“Naiheshimu Azam ni timu nzuri, ila sisi nia yetu ni kuibuka na ushindi ili tutwae ubingwa, hivyo haitakua mchezo rahisi,” alisema Omog.

Kwa upande wake, Cheche alisema wanajua namna ya kuikabili Simba na kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo.

“Mchezo utakuwa mgumu, sisi tumewaona tokea mwanzo kwenye michuano hii na tunawajua tokea huko nyuma, mwalimu waliokuwa naye na sisi tulikuwa naye tunamjua na tunajua ni vitu gani tutafanya, hatuwezi kusema hivi sasa wataviona uwanjani wakati tunacheza.

“Kama tulivyowaahidi mashabiki wetu ushindi, basi na katika mchezo huu wa fainali tutafanya hivyo,” alisema.

Katika maandalizi ya mchezo huo, Simba imekuwa ikifanya mazoezi ya kupiga penalti, mazoezi ambayo tangu wafike Zanzibar hawajawahi kufanya, hali inayotafsiriwa ni kama wameshtuliwa na watani wao Yanga, baada ya mchezo wa nusu fainali kuamuliwa kwa matuta.

Kikosi cha wekundu hao tangu walipotua katika visiwa hivyo na kufanya mazoezi katika Uwanja wa Ngome, hawakuwahi kufanya mazoezi ya kupiga penalti huku zaidi ya kuwa na programu za kawaida.

Hata hivyo, Simba itaendelea kumkosa Fredrick Blagnon katika michuano hiyo kutokana na kuwa majeruhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles