33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MWANAFUNZI ALIYEPEWA UJAUZITO ATISHIWA MAISHA

mimba

Na AHMED MAKONGO-BUNDA

BINTI anayedaiwa kupewa ujauzito na mkazi mmoja wilayani hapa, anadaiwa kupokea vitisho kutoka kwa mtuhumiwa.

Godfrey Mgaya mkazi wa Kijiji cha Karukekere katika Kata ya Namhura Wilaya ya Bunda, mkoani Mara, ambaye ni baba mzazi wa mwanafunzi wa kidato cha pili anayedaiwa kupewa ujauzito na  Zephania Mfungo, amedai binti yake kupewa vitisho na ndugu wa mtuhumiwa.

Kwa mujibu wa Mgaya, ndugu wa mtuhumiwa wamekuwa wakimtishia binti yake wakidai ikiwa  watang’ang’ania suala hilo kulipeleka  kwenye vyombo vya sheria watamfanyia kitu kibaya.

Akizungumza na MTANZANIA Jumamosi jana, Mgaya alisema kwa sasa hivi mtoto wake anaishi kwa wasiwasi kwa hofu ya maisha yake.

Alisema licha ya Mkuu wa Wilaya ya Bunda, Lydia Bupilipili, kuliagiza Jeshi la Polisi wilayani humo kuhakikisha wanamkamata Mfungo pamoja na mwenyekiti wa kijiji hicho, Nyandago Magesa, aliyewazuia askari mgambo kumkamata mtuhumiwa huyo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni rafiki yake, lakini bado watu hao hawajakamatwa.

Mzazi wa mtoto huyo alisema binti yake ambaye ni mwanafunzi aliyekuwa anasoma katika kidato cha pili katika shule ya sekondari Muranda, alifukuzwa shule mwaka jana kutokana na kupewa ujauzito huo na mwanamume huyo, sasa anaishi maisha ya wasiwasi kutokana na vitisho anavyopewa vya kutaka kuuawa.

“Nilikwenda kutoa taarifa ya mwanangu kupewa mimba na huyo mwanamume katika ofisi ya kijiji na kwenye kata, lakini tulipopewa askari mgambo kwenda kumkamata mwenyekiti wa kijiji hicho, Nyandago Magesa, aliwazuia mgambo hao eti wasimkamate kwa sababu ni rafiki yake,” alisema.

Alisema pamoja na kufuatilia suala hilo ili mtuhumiwa huyo akamatwe na kufikishwa mahakamani, lakini kumekuwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na binti yake kutishiwa maisha yake, kwamba iwapo akithubutu kusema ukweli hiyo mimba yake hawezi kujifungua salama na ataondolewa uhai wake.

“Sasa kibaya zaidi tangu tukio hilo liwepo kuna ndugu yake na huyo mtuhumiwa amekuwa akimtishia mwanangu kwamba akitoa taarifa juu ya mimba yake hatajifungua salama na hata wanaweza kumkodishia gari iweze kumgonga wakati akitembea barabarani,” alisema.

Kwa upande wake diwani wa kata hiyo, Jogoro Amoni, alisema suala hilo amelifuatilia sana, lakini bado mtuhumiwa huyo hajakamatwa na kuna madai kuwa alikwenda kujiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) mwaka jana.

Diwani huyo aliiomba Serikali kutenda haki kuhusu sakata hilo, maana suala la wanafunzi kupewa mimba linapingwa vikali na Serikal.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Ramadhani Ng’anzi, alisema tukio hilo bado hajalipata rasmi na kwamba kwa sasa yuko nje ya ofisi lakini atalifuatilia na kuchukuwa hatua zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles