27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NDALICHAKO ASITISHA AJIRA WALIMU WA SANAA

Waziri wa Elimu,Sayansi Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, akizungumza na wakuu wa Shule za Sekondari nchini wakati akifungua mkutano mkuu wa Umoja wa Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari(Tahossa), Dodoma jana.
Waziri wa Elimu,Sayansi Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, akizungumza na wakuu wa Shule za Sekondari nchini wakati akifungua mkutano mkuu wa Umoja wa Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari(Tahossa), Dodoma jana.

Na RAMADHAN HASSAN, DODOMA

WAZIRI wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, ametoa masharti mapya ya ajira za ualimu nchini, huku akisema Serikali haitaajiri walimu wa masomo ya sanaa (arts) kwa kuwa wapo wa kutosha.

Akizungumza mjini Dodoma jana wakati akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA), Profesa Ndalichako, alisema Serikali kwa sasa haiwezi kuajiri walimu wa masomo hayo kwa kuwa inataka kuajiri walimu wa masomo ya sayansi na hisabati ambao idadi yao ni ndogo.

“Pamoja na uamuzi huo mpya, ajira za walimu wapya wa masomo ya sayansi nazo zimebadilika kwani wale wote waliohitimu ualimu wa sayansi na hisabati, wanatakiwa watume vyeti vyao kabla ya kupangiwa kituo cha kazi.

“Kuhusu wale walimu wa ‘arts’, kule tuna walimu wa ziada ambao tutajaribu kuwapanga kutokana na shule, kwani wengi walikuwa wamepangwa shule moja. Kwahiyo, tutaangalia utaratibu wa kuwapanga kulingana na mahitaji,’’ alisema Profesa Ndalichako.

Akizungumzia suala la ubora wa elimu nchini, Profesa Ndalichako aliwataka walimu wakuu hao kuhakikisha wanasimamia ubora wa elimu kwa kuwa wao ndio wanaowaandaa wanafunzi kabla hawajaenda vyuoni.

“Vilevile pelekeni takwimu sahihi za wanafunzi waliopo katika shule zenu kuisaidia Serikali katika kupanga bajeti ili iweze kutoa fedha sahihi.

“Hapa kuna kimbembe, yaani wakati mwingine huwa najifanya nimepoteza takwimu ya shule fulani, nikiziomba na kutumiwa, zinakuwa ni tofauti na zile za mwanzo.

“Hili nawaomba mkalisimamie ili iwe rahisi kwetu kupanga bajeti yenye tija,’’ alisema.

Kuhusu ujenzi wa maabara katika shule za sekondari, waziri huyo alisema kwamba kutokana na nyingi kukamilika, Serikali itatoa vifaa vya maabara kuanzia Januari mwakani baada ya kuwa vimeingia nchini kutoka vilikoagizwa.

Awali, akisoma risala ya walimu hao, Rais wa TAHOSSA, Bonus Nyimbo, aliiomba Serikali itoe waraka wa kupiga marufuku matumizi ya simu kwa wanafunzi shuleni kwa kuwa zimekuwa zikichangia kushuka kwa ufaulu kwa baadhi ya wanafunzi.

“Ili kuboresha elimu, tunaiomba Serikali itoe waraka wa kupiga marufuku matumizi ya simu kwa wanafunzi kwani simu nyingi tunazozikamata tunakuta mule hakuna taaluma,’’ alisema Nyimbo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Global Education Link, Abdulmalik Molel, ambaye pia kampuni yake ilipewa tuzo ya heshima katika kuendeleza elimu nchini, alisema ni jukumu la kila mmoja kutimiza wajibu wake ili kuiendeleza elimu ya Tanzania.

“Kila mmoja anapaswa kutimiza wajibu, wazazi, walezi na walimu, waambieni wanafunzi wasiwe na ‘expectation’ (matarajio) makubwa kwani wanapokuwa na matarajio hayo, wakienda vyuo vikuu wanakuwa wasumbufu,” alisema.

Wakati hayo yakiendelea, juzi taarifa ilitolewa jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Maimuna Tarishi, ikisema kwamba, walimu wahitimu wa masomo ya sayansi na hisabati waliohitimu shahada na astashahada mwaka 2015, wanatakiwa kuwasilisha nakala za vyeti vya elimu ya sekondari vya kidato cha nne na sita na taaluma ya ualimu kwa uhakiki.

Pamoja na hayo, hivi karibuni Serikali ilitangaza kusitisha ajira zote nchini ili kukabiliana na wimbi la watumishi hewa.

Sambamba na uamuzi huo, nyongeza za mishahara kwa watumishi wa Serikali nazo zilisimamishwa ili kukabiliana na watumishi hao hewa ambao walikuwa wakiingizia hasara Serikali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles