29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Askari JWTZ mbaroni kwa tuhuma za wizi wa mtoto

kamanda-wa-polisi-mkoa-wa-taborakhamis-issaNa Kulwa Karedia

POLISI mkoani Tabora inamshikilia askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ),kwa tuhuma za kuiba mtoto mchanga,Razack Kombo, mwenye umri wa miezi miwili.

Habari za uhakika ambazo MTANZANIA ilizipata jana na kudhibitishwa na Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Tabora,Khamis Issa, zinasema askari huyo wa Kikosi cha Jeshi Mirambo, anashikiliwa baada ya kichanga hicho kufariki dunia katika mazingira ya kutatanisha.

“Tunamshikilia askari huyo tangu wiki iliyopita kwa kosa la wizi wa mtoto mchanga ambaye pia alifariki dunia katika hali iliyojaa utata ingawa bado tunaendelea kufanya mahojiano naye ili atueleze namna hali ilivyokuwa.

“Hivi ninavyoongea na wewe niko nje ya ofisi,lakini wasaidizi wangu wamenijulisha wamemkamata.Haiingii akilini mtu aibe kichanga hiki alafu kipoteze uhai ndani ya muda mfupi, tena mwili wake umekutwa kwenye moja ya hospitali ya jeshi,japokuwa taarifa zinaonyesha alikuwa haumwi.

“Kama ningekuwa ofisini, ningeweza kukutajia namba za askari huyo pamoja na majina kamili kwa sababu tunayo.

“Lakini, nakuomba univumilie kama nitawahi kurudi ofisini, tutawasiliana zaidi.

“Katika mahojiano ya awali, askari huyo alisema alikuwa anakwenda likizo ya uzazi nyumbani kwao,japo hakuwa na ujauzito.

“Inaonekana mama wa mtoto aitwaye Daphina Matwika, alikuwa anasafiri kutoka Morogoro kwenda Mpanda kule Katavi akiwa na watoto wengine wakubwa wawili.

“Kwa hiyo, baada ya kutokea wizi huo, mama wa mtoto alikwenda kutoa taarifa kituo cha polisi cha stendi kuu ya mabasi Tabora ambapo polisi walianza kuweka mitego iliyosaidia kumnasa askari huyo,” alisema Kamanda Issa.

Baada ya kumkamata askari huyo, Kamanda Issa alisema waliwasiliana na mama wa marehemu ambaye tayari aliyekuwa amefika  Mpanda na aliporudi, alimtambua mtoto huyo.

“Baada ya utambuzi wa mwanamke huyo, uliibuka mvutano kati yake na askari huyo kwani kila mmoja alikuwa akidai mtoto ni wake.

“Tulichokifanya ni kuwafanyia kipimo cha kuwachukua damu na kutuma vipimo hivyo kwa Mkemia Mkuu wa Serikali,” alisema.

 

Mama asimulia

 

Akizungumza na MTANZANIA jana kutoka Mpanda, mama wa marehemu alisema ameumizwa na tukio hilo na sasa yupo katika wakati mgumu.

“Nakumbuka Jumatatu wiki iliyopita nilipanda basi la Kampuni ya NBS pale Msamvu Morogoro, nikiwa na watoto wangu watatu akiwamo marehemu nikielekea Mpanda.

“Safari yetu ilianza kupata matatizo tulipofika Dodoma kwa sababu basi lilikamatwa na dereva aliwekwa ndani karibu saa nne hivi kwa sababu alipishana lugha na trafiki.

“Baadaye tuliondoka Dodoma kwenda Tabora ambako tulifika saa 3:30 usiku.

“Wenye basi walituteremshia ofisini kwao badala ya stendi. Kwa hiyo, nilichukua teksi hadi stendi kuu ambapo nilitafuta nyumba ya kulala wageni nikakosa.

“Tuliamua tulale pale pale stendi na wakati wote huo, yule dada alikuwa pembeni yangu ananiangalia tu.

“Ilipofika majira ya saa saba usiku, alinifuata nilipokuwa nimelala akaniambia niinuke niende alipo lala yeye kwa sababu ameweka mkeka, lakini nilimkamtalia.

“Cha ajabu ilipofika saa 10 alfajiri, alikuja tena akaniomba anisaidie kubembeleza mtoto kwa sababu alikuwa analia, lakini pia nilikataa kisha aliniambia twende uani, pia nikakataa.

“Nilipomkatalia, aliondoka kisha akarudi,akaniomba tena mtoto nikamkatalia na wakati huo nikamkabidhi mwanangu mkubwa yule mtoto mimi nikaenda uani.

“Inaonekana nilipokwenda uani tu, alimwambia mwanangu mkubwa wasogee mbele, ghafla akamwambia arudi aangalie mabegi yasiibiwe huku akiwa na mtoto, sasa aliporudi ndiyo akatoroka pale na yule mwanangu mdogo,”alisema Daphina.

Baada ya tukio hilo, alisema alipiga kelele kuomba msaada na baadaye akaambiwa akatoe taarifa polisi kwa msaaad zaidi.

” Nashukuru kwa ushirikiano nilioupata kutoka kwa askari kwani walinisaidia kumpata mtuhumiwa pamoja na mwili wa marehemu mwanangu uliokuwa umehifadhiwa katika Hospitali ya Jeshi Mirambo,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles