Na TUNU NASSOR-ALIYEKUWA PWANI
WAKAZI wa Kijiji cha Tundu, Kata ya Bupu, Mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na Mbunge wa Mkuranga, Abdallah Ulega (CCM), wameamua kufyatua matofali kwa ajili ya kujenga zahanati.
Wananchi hao wamelazimika kuchukua uamuzi huo, baada ya kuwa wanatembea kilomita zaidi ya tisa kufuata huduma za afya.
Akizungumzia uamuzi huo mwishoni mwa wiki, Ulega alisema uamuzi huo umefikiwa ili kuleta mabadiliko jimboni humo.
“Wananchi wangu wanatembea umbali mrefu kufuata huduma za afya, jambo ambalo linawafanya wapate tabu pindi wanapougua.
“Kwa kuwa nia yangu ni maendeleo, naahidi kushirikiana nao bega kwa bega katika hili ili hata nikimaliza muda wangu wa uongozi, iwepo kumbukumbu juu ya kile nilichokifanya kwa wananchi.
“Kwa hiyo, nawaomba sana ndugu zangu tushikamane katika hili, tuunge mkono viongozi wetu hasahasa Rais Dk. John Magufuli ambaye amekuwa akihimiza maendeleo kila siku.
“Katika hili, naomba tuondoe itikadi zetu, wasiokuwa wana CCM na wanachama wa vyama vingine vya siasa, tuwe kitu kimoja ili tuweze kupata maendeleo kwa haraka,” alisema Ulega.
Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho, Nassoro Mzindu, alisema kijijini kwake kuna matatizo ya huduma za kijamii ikiwamo ukosefu wa huduma ya afya, miundombinu, pamoja na maji.
“Tuna matatizo mengi sana yanayohitaji ufumbuzi, kwa hiyo mimi kwa niaba ya wananchi ninaowaongoza, tuko pamoja na mbunge wetu katika suala la maendeleo,” alisema Mzindu.
Naye mmoja wa wakazi wa kijiji hicho, Mshamu Lilenga, aliunga mkono jitihada za kujenga zahanati hiyo kwa kuwa itawasaidia kuimarisha afya zao.