Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
KAMPUNI ya mafuta ya Puma imezindua mfumo maalumu wa kununua mafuta kwa kutumia huduma mpya ijulikanayo kama ‘Airtel Money Tap Tap’ ambayo humwezesha kupata huduma hiyo katika kituo chochote nchini.
Akizungumza katika uzinduzi huo juzi Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa Puma Energy Tanzania, Philippe Corsaletti, alisema wana jukumu la kuhakikisha huduma wanazozitoa kwa ajili ya Watanzania zinakuwa salama wakati wote, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano za kuhamasisha kutumia njia za kieletroniki kwenye malipo ya fedha.
Alisema kadi hiyo itamwezesha mteja pindi anapotaka kununua mafuta kwa kutumia kadi ya Airtel badala ya kutoa fedha taslimu akiwa kituo cha mafuta.
Alisema wanahisi kwamba wanawajibu wa kufanya huduma zao kwa usalama, zenye ufanisi na rahisi zaidi kwa wateja wao na kufafanua ni hatari kubeba fedha wakati wote maana ni rahisi kuhatarisha maisha.
Aidha, alisema ili kuhakikisha jamii ya Watanzania inakuwa salama wakati wote, kuna haja ya kuwa na huduma hiyo ambayo itamuwezesha anayehitaji kununua mafuta kwenye vituo vya Puma vilivyopo maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam wanatumia kadi za Airtel kununua mafuta.
“Milango yetu iko wazi kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma zetu na tunaweza kufanya jambo lolote ili kuhakikisha jamii yetu inakuwa salama wakati wote. Hivyo, kuna umuhimu wa kuwa na matumizi ya kadi ya Airtel katika kununua mafuta kwenye vituo vyetu vya Puma.
“Kadi hii imeundwa kwa namna ambayo wakati wa kutumika kufanya malipo, hupunguza fedha kwa kiasi cha malipo kutoka katika akaunti ya Airtel Money ya mnunuzi kwenda kwenye akaunti ya muuzaji. Kadi hii itakuwa inauzwa kwa bei ya Shilingi 2, 000 kwenye vituo vyote vya Puma Dar es Salaam na maduka yote ya Airtel Tanzania,” alisema.
Alitumia nafasi hiyo kueleza kuwa Puma Tanzania ina jumla ya vituo 46 nchini kote na kwa kuanza, vituo vyote vya Dar es Salaam vitakua vinatoa huduma hiyo na vilivyosalia vitaunganishwa kuanzia mapema mwakani.