24.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Lipumba, Maalim Seif jino kwa jino

ZIFF chief guest, 1st vice president, Maalim Seif Sharif at ZIFF 2013*Kutinga ofisini kwake Buguruni

*Kusindikizwa na wabunge na mameya

Na Patricia Kimelemeta

-DAR ES SALAAM

NI jino kwa jino. Ndivyo unaweza kusema hasa baada ya Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, kutarajiwa kuripoti ofisini kwake Buguruni  Dar es Salaam huku Mwenyekiti wa chama hicho aliyerejeshwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba, akitangaza kumpokea kiongozi huyo.

Hatua hiyo inatokana na maswahiba hao wa miaka mingi    kugeuka maadui ambao kwa sasa ‘hawapikwi chungu’ kimoja hata kufikia kufukuzana ndani ya chama hicho.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Kaimu Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Uhusiano wa Umma, Mbarara Maharagande, alisema  kesho  Maalim Seif ataripoti ofisini kwake Buguruni akisindikizwa na wanachama na viongozi wa chama hicho.

Alisema mapokezi hayo yatawajumuisha wanachama wa CUF wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kushirikiana na wabunge.

Katika mapokezi hayo  watawakaribisha wajumbe wa Baraza Kuu Ofisi Kuu ya CUF Buguruni baada ya kumaliza kazi kubwa ya kutengeneza mustakabali wa chama.

“Wanachama wa CUF wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa kushirikiana na wabunge wote wa CUF, wameandaa mapokezi haya makubwa yatakayofanyika kesho Ijumaa Septemba 30  kuanzia saa 2.00 asubuhi.

“Watawakaribisha wajumbe wa Baraza Kuu la Uongozi Taifa katika Ofisi Kuu za CUF Buguruni.

“Wajumbe hao watakuwa wanatoka Zanzibar kwenye kikao maalumu kilichotengeneza mustakabali muhimu wa chama na  mameya wa CUF, madiwani, Kamati ya Uongozi ya chama, Katibu Mkuu (Maalim Seif) wote watakuwapo.

“Mbali na hao pia watakuwapo wakurugenzi, wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya chama na watu   muhimu ambao kwa pamoja watafika Buguruni na kuanza kazi,” alisema Maharagande

Kauli ya Lipumba

Akizungumza na waandishi wa habari   Dar es Salaam jana, Profesa Lipumba  alisema atampokea Maalim Seif siku yoyote atakayofika na  pamoja na mambo mengine atapanga naye mikakati ya ujenzi wa chama.

Alisema CUF inamtambua Maalim Seif kama Katibu Mkuu, hivyo basi hawezi kumtenga atakapofika kwenye ofisi hizo zilizopo Buguruni kwa sababu kuna ofisi yake ya kufanyia kazi.

“Namsubiri Maalim Seif aje kwenye ofisi zetu za Buguruni ili tukae na kukijenge chama kwa sababu anatambua kuwa mimi ni mwenyekiti halali kwa mujibu wa Katiba yetu. Kinachojitokeza sasa ni migongano ya siasa ambayo inaweza kumalizika wakati wowote.

“Naamini siku atakayokuja tutampokea na kumpeleka ofisini kwake kwa ajili ya kuchapa kazi, lakini pia nitampa mwongozo wa namna ya kukijenga chama ikiwa ni pamoja na kumwambia kuwa fedha zisitutenganishe,”alisema Prof. Lipumba.

Akizungumzia kikao cha Baraza Kuu kilichofanyika Visiwani Zanzibar ambacho pamoja na mambo mengi kilitangaza kumvua uanachama,  a alisema kikao hicho ni batili na kimekiuka katiba ya chama hicho.

Alisema kikao chenye wajibu wa kumfukuza uanachama ni Mkutano Mkuu pekee ambao unawashirikisha  wajumbe wote kutoka kila upande   wa Bara na Zanzibar.

“Kifungu cha 79(2)(a) cha Katiba ya chama hicho kinasema kuwa, Mkutano Mkuu   unaweza kuchukua hatua za nidhamu zozote zile zikiwamo kumuachisha au kumfukuza uongozi au uanachama au yote mawili, mwenyekiti wa chama hicho.

“Mimi navuliwa uanachama na Mkutano Mkuu, siyo baraza la uongozi ambalo na lenyewe halijakidhi matakwa ya katiba ya chama… kilichofanyika Zanzibar ni sawa na kikao cha harusi,” alisema.

Alisema licha ya kufanyika   kikao hicho,   pia idadi ya wajumbe waliohudhuria kutoka upande wa bara ni tisa kati ya 22 na wajumbe watatu ni wakurugenzi huku wanachama wa kawaida walikuwa sita.

Profesa Lipumba alisema kwa mujibu wa Katiba ya CUF, kikao cha Baraza Kuu huitishwa na mwenyekiti na hutakiwa kukutana kila baada ya miezi minne isipokuwa kama kuna dharura.   Linakutana chini ya mwenyekiti na si vinginevyo, alisisitiza.

“Kifungu cha 83(1) ambacho kinalipa mamlaka Baraza Kuu kuwasimamisha uongozi na siyo kuwavua uanachama viongozi wakuu  wa chama   ambao ni Mwenyekiti, Makamu na Katibu Mkuu.  Hivyo baraza halina uwezo wa kunivua uanachama,” alisema.

Alisema katiba hiyo, kifungu cha 83(5) kinasema, baraza hilo linaweza kuchukua hatua za nidhamu ikiwa ni pamoja na kutoa onyo kwa maandishi na karipio kali.

Alisema hakuna hatua zilizofuatwa katika Baraza Kuu hasa kwa kumvua uanachama  ila kuna fitina zinazochochewa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema).

“Mimi sifukuziki ndani ya chama hiki, wala sisusi, nimelipia kadi yangu hadi mwaka 2020, nitaendelea kukipigania chama hiki hadi mwisho, sihami, siondoki…wala siendi mahakamani, nipo ngangari, wakija Buguruni watanikuta kama mwenyekiti wa chama,” alisema.

Juzi, Baraza Kuu la Uongozi la CUF lilitangaza kumvua uanachama Profesa Lipumba kwa kile kilichoelezwa kukaidi wito wa kwenda kujieleza kwa kuvamia ofisi za CUF za Buguruni na kufanya uharibifu wa mali za chama.

Septemba 23, Msajili wa vyama Jaji, Francis Mutungi, alimrejesha katika nafasi yake ya uenyekiti na siku iliyofuta kiongozi huyo alikwenda ofisini kwake Buguruni na kuzuka tafrani hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles