JOHANES RESPICHIUS-Dar es Salaam
KAMANDA wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro, amesema viongozi wa juu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliotakiwa kuripoti jana katika Kituo Kikuu Polisi badala yake wataripoti Septemba 6, mwaka huu.
Viongozi hao ni pamoja na Mwemyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, Mjumbe wa Kamati Kuu, Edward Lowassa, Katibu mkuu, Vincent Mashinji, Naibu wake, John Mnyika na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Said Issa Mohammed.
Akizungunmza na MTANZANIA kwa simu, Sirro, alisema jeshi hilo linajua kuwa viongozi hao wa Chadema wanatakiwa kuripoti kituoni hapo Jumanne ijayo.
“Tumewaambia waripoti hapa kituoni siku ya Jumanne wiki ijayo… kuhusu kwa nini haikuwa leo waulize wao waliotakiwa kuripoti,” alisema.
Viongozi hao wa Chadema walikamatwa na polisi hivi karibuni wakiwa katika kikao maalum cha Kamati Kuu katika Hoteli ya Giraffe Dar es Salaam. Walihojiwa na kutakiwa kuripoti jana katika kituo hicho.
Hata hivyo gazeti moja linalotolewa kwa njia ya mtandao (jina tunalo) lilimkariri Kamanda Sirro akisema kuwa baada ya Chadema kutangaza kusimamisha maandamano yao maarufu kama Ukuta, Jeshi la Polisi liliwataka waliokamatwa juzi kutokwenda kuripoti polisi.