31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Vyuo vikuuu vinavyotoza ada kubwa duniani

Chuo Kikuu cha Columbia
Chuo Kikuu cha Columbia

NA FARAJA MASINDE,

ELIMU imekuwa na gharama kubwa mno, ambapo kila kukicha inazidi kupanda thamani.

Ni kweli kuwa kila mmoja anahitaji kupata elimu kwenye maisha yake kwa lengo moja la kufanikiwa kimaisha kwa kupata kazi nzuri yenye maslahi.

Kwa miaka ya hivi karibuni, eneo la elimu ya juu limekuwa na ushindani mkubwa ambapo kila chuo kinajitahidi kuweka miundombinu rafiki kwa ajili ya kuhakikisha kinakuwa ngwiji katika utoaji elimu ya juu.

Kuna vyuo ambavyo vimekuwa na majina makubwa duniani kote mpaka kuchangia wanafunzi karibu kila pembe ya dunia kuvikimbilia.

Vyuo vikuu kama Cambridge, Yale, Harvard au Oxford ni kati ya vyuo vyenye mvuto mkubwa zaidi duniani achilia mbali heshima ambayo vimekuwa vikipata kila kukicha, inayotokana na majina makubwa ya wanafunzi waliowahi kusoma hapo ambao wengi wao ni viongozi wakubwa wa duniani.

Hii ni orodha ya vyuo vikuu vitano vinavyoshika rekodi ya kutoza kiwango kikubwa cha fedha kwa maana ya ada kwa mwaka.

Wesleyan- Dola 58,500

Chuo hiki kimekuwa kikitambulika na kusifika zaidi duniani kutokana na kiwango cha taaluma kinachotolewa pamoja na mitaala bora.

Wanafunzi hupewa fursa ya kujifunza shughuli za uzalishaji pamoja na kuwaunganisha na taasisi mbalimbali achilia mbali kuwajengea uwezo wa kujitegemea na kufanya kazi.

Hata hosteli za wanafunzi wanaosoma katika chuo hiki ni za hali ya juu kwa maana ya mandhari, pia mwanafunzi hupewa uhuru wa kuchagua kitu anachotaka kushiriki.

Inaelezwa kuwa hata idadi kubwa ya waongozaji mashuhuri wa filamu katika kiwanda cha filamu cha Hollywood nchini Marekani, wamehitimu katika chuo hiki. Ndio maana hata filamu zao zimekuwa na mvuto mkubwa duniani kote.

Columbia – Dola 58,742

Chuo hiki kilianzishwa mwaka 1754 kama chuo kikuu cha Mfalme Georgr wa pili wa Uingereza.

Kinashika nafasi ya 50 katika vyuo vikuu vikongwe nchini Marekani kikiwa cha kwanza kwenye mji wa New York.

Jina lake kamili ni Chuo Kikuu cha Columbia kilichoko katika mji wa New York, japo kimekuwa kikitambulika zaidi kama Chuo Kikuu cha Colombia.

Kimetoa wahitimu wengi mashuhuri duniani ambapo miongoni mwao ni Rais wa Marekani, Barack Obama.

Harvey Mudd – Dola 58,913

Chuo hiki ni moja ya vyuo bora vinavyotoa taaluma ya uhandisi wa Sayansi na Mahesabu nchini Marekani.

Kwasasa kinatoa fursa kwa wanafunzi kujifunza na kushughulikia masuala ya mazingira na katika mitazamo mbalimbali bila kubadilisha taaluma zao.

Kilianzishwa mwaka 1955 kupitia msaada uliotolewa na familia ya Harvey Mudd, kitu kinachaovutia kuhusu chuo hiki ni kiwango cha mshahara wa kuanzia ambapo kwa wastani kima cha chini ni kati ya dola za Marekani 75,000 hadi 80,000 pindi unapopata nafasi ya kufundisha hapa.

New York – Dola 59,337

Hiki kilianzishwa mwaka 1831 kikiitwa City of New York na baadaye mwaka 1896 kilibadilishwa jina na kuitwa Chuo Kikuu cha New York.

Kinawakilisha moja ya vyuo ambavyo vinaongoza kwa kutafutwa zaidi kwenye mitandao na wanafunzi wa kimataifa.

Pia kimepokea tuzo za Taifa za medali za sayansi mara 10, huku kikishinda medali 36 za Nobel.

Sifa nyingine ya chuo hiki ni kwamba hakina kampasi na hivyo wanafunzi muda mwingi wamekuwa chuoni hapo.

Sarah Lawrence – Dola 61,236

Chuo Kikuu cha Sarah Lawrence ni huria na kinamilikiwa na mtu binafsi. Kinatoa taaluma ya sanaa huko mjini Westchester, Yonkers (New York) Marekani.

Kilianzishwa mwaka 1926 na William van Duzer Lawrence na kukipa jina la mkewe, ambaye ni Sarah.

Pia ni miongoni mwa vyuo vilivyotoa watu maarufu na mashuhuri duniani wakiwamo Sigourney Weaver, Barbara Walters, J.J. Abrams na Vera Wang, ambao ni wabunifu maaarufu duniani.

Kwa mwanafunzi yeyote duniani sehemu ya uchaguzi wa chuo cha kusoma ni jambo la busara mno.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles