WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amekataa kupokea msaada wa madawati uliotolewa na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) baada ya kubaini yametengenezwa chini ya kiwango.
Tukio hilo lilitokea jana mkoani hapa baada ya kuwasili katika Kiwanja cha Mabau, Mtibwa, kwa ajili ya kuzungumza na wananchi ambako alikabidhiwa madawati hayo na Meneja wa TFS.
“Ofisa elimu njoo kagua haya madawati yaliyo mazuri nitayapokea na yaliyobaki yarudishwe karakana yakatengenezwe upya, huu si wakati wa kupokea vitu vibovu,” alisema Majaliwa.
Alisema anatambua dhamira ya TFS ya kuunga mkono jitihada za Serikali za kumaliza tatizo la upungufu wa madawati lakini hawezi kupokea madawati yaliyotengenezwa chini ya kiwango.
Baada ya Ofisa Elimu (Msingi) wa Wilaya ya Mvomero, Michael Ligola kukagua madawati 102 yaliyoletwa uwanjani hapo, madawati 84 yalibainika kuwa ni mabovu na 14 tu ndiyo yalikuwa mazima.
Kutokana na hali hiyo, Majaliwa alisema hawezi kupokea madawati hayo yaliyotolewa na Meneja wa Msitu wa Mtibwa, Hamza Kateti na kuuagiza uongozi wa wilaya ufuatilie suala hilo kwa kuwa walitakiwa kuyakagua kabla ya yeye kukabidhiwa.
Vilevile, aliwasisitiza wazazi na walezi wa wilaya hiyo kuhakikisha wanawapeleka watoto wao shule na atakayeshindwa atachukuliwa hatua kali za sheria.
“Serikali imewapunguzia mzigo kwa kuwaondolea michango na ada hivyo tumieni fursa hiyo kwa kuwapeleka shule watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule na wasimamie masomo yao,” alisema.