Na Ibrahim Yassin, Tunduma
MAUAJI yanayohusishwa na imani za ushirikina mkoani Songwe yameongezeka kwa kasi hali iliyosababisha Kamati ya Ulinzi na Usalama kukutana kujadili itakavyokabiliana na hali hiyo.
Hilo lilibainishwa na wakazi wa Songwe kwa nyakati tofauti na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo.
Baadhi ya wananchi hao,Ajuaye Dimai na Elly Makenge kwa nyakati tofauti, walisema vimekuwapo vitendo vya mauaji ya kinyama vya watu wananyofolewa baadhi ya viungo vya sehemu za miili yao, mauaji yanayodaiwa kufanywa kwa imani za kupata utajiri.
“Watu wanaofanya mauaji haya wamekuwa wakisaka utajiri kwa nguvu, wakitumia ushirikina kwa kuhitaji viungo vya binadamu yakiwamo macho, ulimi, vidole, moyo na vinginevyo, ambavyo wanavipeleka kwa waganga wa kienyeji.
“Kuna baadhi ya waganga wa kienyeji wanawarubuni wafanyabiashara kupeleka viungo wawatengenezee dawa kwa lengo la kupata utajiri. Serikali isipochukua hatua hali itakuwa mbaya,”alisema Makenge.
Kamanda wa Polisi mkoani Songwe, Mathias Nyange, alisema ni kweli mauaji ya aina hiyo yamekuwa yakiendelea.
Alisema zikipita saa sita hajapokea taarifa za mauaji ya aina hiyo siku hiyo hulala usingizi mzuri.
Nyange alisema kila siku zimekuwapo taarifa za mauaji katika kila wilaya za mkoa huo.
Alisema katika uchunguzi wa polisi imebainika kuwapo baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu wanaoendesha vitendo hivyo kwa imani ya kupata mafanikio.
Hata hivyo, Kamanda Nyange, alisema polisi wanajipanga kuendesha semina elekezi kwa wananchi kwa kushirikiana na viongozi wa Serikali za vijiji kuwapa uelewa wananchi waachane na imani hiyo.
“Juzi tu maeneo ya Mbozi tumeokota mwili wa mtu ukiwa umeuawa na kutolewa macho,”alisema.
Mkuu wa Mkoa wa Songwe ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama mkoani humo, Luteni (mstaafu), Chiku Galawa, alisema hata yeye alipofika mkoani humo alipata taarifa za mauaji hayo yanayohusishwa na imani za ushirikina.
Galawa alisema kwa sasa hakuna kulala na watahakikisha wanatembelea vijiji vyote mkoani humo kutoa elimu hiyo jamii ijue wazi kuwa mafanikio hayaji kwa kuua bali ni juhudi za kufanya kazi kwa kujituma.