30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

LULU: Wanaonitukana Instagram fresh tu!

lulu

NA KYALAA SEHEYE,

STORI zilivuma na bado vuguvugu linaendelea kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kuhusu uhusiano wa staa wa kike katika filamu za Kibongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’ na mama Kanumba, Flora Mtegoa kuwa siyo mzuri kama zamani.

Watoa habari wa mjini, wanadai kuwa mama Kanumba na Lulu kwa muda mrefu sasa hawapikiki chungu kimoja kama ilivyokuwa zamani.

Lulu alikuwa mchumba wa mwigizaji wa filamu za Kibongo, marehemu Steven Kanumba ambaye alifariki dunia Jumamosi ya Aprili 07, 2012, nyumbani kwake, Sinza – Vatican jijini Dar es Salaam.

Mbali na mitandao ya kijamii kukuza kinachoitwa bifu kati ya mtu na mkwewe huyo, magazeti mbalimbali yalipata kuripoti kuhusiana na kuwepo kwa kutokuelewana baina yao.

Katika mahojiano na My Style ya Swaggaz ndani ya Mtanzania Jumamosi, Lulu alifunguka mengi kuhusiana na madai ya bifu hilo, akikiri kuwepo lakini akasema kuwa kwa sasa imebaki stori tu.

Akizungumzia hilo anasema: “Ni kweli kuna wakati  kulitokea kutoelewana kidogo na naweza kusema ni jambo la kawaida. Jamani binadamu kutofautiana mitazamo wakati fulani si kitu cha kushangaza.

“Lakini hayo mambo yalishaisha kabisa. Mimi na mama Kanumba tupo vizuri sana kwa sasa. Sina ugomvi naye,  tunaelewana na tunaishi vizuri kabisa. Mikwaruzano ya mwanzo iliisha na tunaendelea vyema.”

Lulu anawaangushia lawama watu wenye tabia za kukuza mambo mitandaoni ambao hawamtakii mema kwa kuzusha kuwa bado wana bifu.

“Tatizo kuna watu hawana kazi za kufanya, kazi yao kushinda mitandaoni na kutunga habari za uongo au kukuza mambo ambayo hayapo. Watu waache, mimi sina tatizo na mama Kanumba.

“Yule ni mtu mzima, nawezaje kuwa na bifu naye? Ninachoweza kusema ni kwamba kulikuwa na kupishana kauli kidogo, lakini hayo mambo yameshaisha, watu wasijaribu kuendelea kukuza,” anasema Lulu ambaye ni mshindi wa Tuzo ya  Africa Magic Viewer’s Choice Awards katika kipengele cha Filamu Bora ya Afrika Mashariki kupitia filamu yake ya Mapenzi ya Mungu ambayo mama Kanumba pia ameshiriki.

MY STYLE: Unapenda kuishi vipi wewe kama staa?

LULU: Kama binti napenda maisha mazuri ndiyo maana najituma ili niweze kufanikiwa. Kama nilivyosema huwa sipendi uzushi na ugomvi, ndiyo maana ninapozushiwa au kutukanwa mara nyingi huwa nanyamaza kwa kuwa sipendi malumbano na watu. Napenda amani.

MY STYLE: Unajivunia nini katika sanaa yako?

LULU: Nimefanikiwa kimaisha nashukuru, pili najivunia kupata tuzo ya kimataifa kule Lagos, Nigeria. Kwangu ni mwanzo mwema na mwanga mzuri mbele yangu.

MY STYLE:  Lulu ana tofauti gani na waigizaji wengine wa Bongo?

MY STYLE: Lulu ni Lulu hawezi kuwa mtu mwingine na mtu mwingine hawezi kuwa Lulu, nadhani hiyo ndiyo tofauti.

MY STYLE: Unazungumziaje skendo zinazokuandama katika mitandao ya kijamii na wale ambao hukushushia matusi?

LULU: Nachukulia kama changamoto tu katika kazi kwani kuna mambo mengine nahusishwa nayo ila siyajui. Ila ninachojua, hao wanaonitukana ndiyo haohao mashabiki wangu, sema wanajibalaguza tu lakini moyoni wananikubali.

MY STYLE: Wewe ni shabiki wa chama gani cha siasa?

LULU: Mimi sina chama, ndiyo maana hata katika kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka jana, sijaonekana kwenye jukwaa lolote. Miye naamini kura ni siri na nilifanya hivyo ili nisifungamane na upande wowote.

MY STYLE: Una ushauri gani kwa mastaa wenzako?

LULU: Tushirikiane na kufanya kazi kwa ufanisi, tuongeze juhudi ili tuweze kurudisha hadhi ya soko la filamu kama lilivyokuwa awali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles