MBUNGE wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema),
jana alifikishwa katika Mahakama ya Mwanzo ya Maji ya Chai wilayani Arumeru kwa tuhuma za uharibifu wa mali.
Mbele ya Hakimu wa Mahakama hiyo, David Mwita, ilidaiwa kuwa Mbunge huyo alitenda kosa hilo juzi jioni katika eneo la Maji ya Chai Kati, nje kidogo ya jiji la Arusha.
Ilidaiwa kuwa Nassari kwa makusudi alichoma bendera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyokuwa na thamani ya Sh. 250,000, kitendo ambacho ni kosa na kinyume cha sheria.
“Mlalamikaji katika kesi hii ni Raphael Mosses ambaye hajafika
mahakamani hapa na mtuhumiwa anadaiwa kuwa kwa makusudi alichoma bendera ya CCM,” yalidai mashitaka hayo.
Alipokamatwa juzi, Mbunge huyo alilala mahabusu hadi jana alipopewa dhamana. Kesi hiyo iliahirishwa hadi Desemba 24 mwaka huu itakapotajwa tena.