27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Singasinga aivimbia Serikali

SeithNa Kulwa Mzee, Dar es Salaam

WAKATI ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ikionyesha Kampuni ya Power Solution Limited (PAP) ilikwepa kodi ya Sh bilioni 8.68, kampuni hiyo imekimbilia Bodi ya Rufaa ya Kodi kupinga hatua ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuondoa hati za awali za kuthibitisha ulipaji wa kodi.

PAP ambayo inadaiwa kulipwa visivyo halali Sh bilioni 306 zilizokuwa kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, ombi lake lilikubaliwa na bodi hiyo ambayo imemzuia kwa muda Kamishna Mkuu wa TRA kuondoa hati zake zinazothibitisha ulipwaji wa kodi wakati wa mchakato wa kununua hisa za Kampuni ya IPTL.

Uamuzi huo ulitolewa Novemba 26 na Katibu wa bodi hiyo, Respicius Mwijage, baada ya kusikiliza maombi ya zuio la muda yaliyowasilishwa na PAP na IPTL dhidi ya Kamishna Mkuu wa TRA na Msajili wa Makampuni nchini (Brela).

Madai ya msingi ya PAP ni kutaka kuendelea kutambulika kama kodi waliyolipa ni halali na kupinga uamuzi wa TRA kuondoa hati zake hizo.

Katika kutaka zuio la muda, wadai hao waliitaka bodi hiyo iwazuie walalamikiwa, mawakala wao, waajiri wao au mtu yeyote atakayefanya kazi kwa niaba yao kuondoa hati za kuthibitisha kulipwa kwa kodi ya ongezeko la mtaji kuhusu uuzwaji wa hisa za IPTL.

Katika maombi hayo, wadai walizitaja hati hizo kuwa ni namba 0049656 na 0049657 ambazo zilitolewa kwa ajili ya uuzaji wa hisa kutoka Kampuni ya Mechmar na Piper Links Investment na kati ya Piper Links na PAP.

Walitaka hati hizo zizuiwe kuondolewa kwa namna yoyote hadi rufaa waliyofungua kupinga kuondolewa itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

Kampuni hiyo pia inaiomba bodi itoe amri ya muda kwamba hali ilivyo sasa iendelee kuwa hivyo hadi rufaa yao itakaposikilizwa.

Madai hayo yaliambatana na hati ya kiapo iliyoapwa na Manraj Bharya ambaye ni Mkurugenzi wa PAP na Parthiban Chandrasakaran ambao wanadai katika kiapo kwamba PAP ilishanunua hisa zote za IPTL.

Hati hiyo ya kiapo inadai Novemba 19 Kamishna wa TRA alitoa taarifa kwa IPTL akionyesha nia ya kuondoa hati hizo zinazothibitisha kuwa kampuni hiyo ililipa kodi.

Inadaiwa sababu za kuondoa hati hizo ni kutokana na mkataba feki wa makubaliano ya mauzo ya hisa hizo kwa makampuni husika ambapo kodi iliyolipwa inaonekana ilikuwa ndogo.

Wadai hao waliiomba mahakama kutoa zuio la muda kwani isipofanya hivyo wataingia kwenye hasara ambayo haiwezi kulipika.

Hata hivyo, Katibu Mwijage alitoa amri ya muda kwamba hali ibaki kama ilivyo sasa na kwamba nia ya kuondoa hati za kuthibitisha ulipaji wa kodi iliyotolewa na TRA kupitia barua ya Novemba 19 mwaka huu ikielekezwa BRELA, isimamishwe hadi maombi yatakaposikilizwa.

Aliamuru maombi ya kuwazuia TRA na BRELA kuondoa hati za ulipaji kodi yasikilizwe Desemba 10.

RIPOTI YA CAG NA KODI ILIYOKWEPWA

Kwa mujibu wa ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Septemba 9, 2012 Kampuni ya Mechmar iliuza hisa saba kwa Piper Links ilizokuwa inamiliki katika Kampuni ya IPTL kwa bei ya dola za Marekani milioni 6.

Hata hivyo, taarifa zilizowasilishwa TRA kwa ajili ya kukokotoa kiasi cha kodi ya ongezeko la mtaji ambacho Mechmar ilitakiwa kulipa, zinaonyesha hisa hizo zimeuzwa kwa Sh milioni 6 za Kitanzania badala ya dola za Marekani.

Kutokana na udanganyifu huo, kodi ya ongezeko la mtaji iliyolipwa ni Sh 596,500 badala ya Sh 1,919,988,800 iliyopaswa kulipwa.

Kwa upande wa ushuru wa stempu, Mechmar ilipaswa kulipa Sh milioni 96 na siyo Sh 60,000 ilizolipa.

“Jumla ya kodi iliyopotea kwa maana ya kodi ya ongezeko la mtaji na ushuru wa stempu ni Sh 2,015,988,800,” inasema taarifa ya PAC.

Inasema hisa hizo kutoka Kampuni ya Piper Links kwenda PAP, ziliuzwa kwa gharama ya dola za Marekani milioni 20, lakini taarifa zilizopelekwa TRA zilionyesha hisa hizo zimeuzwa kwa dola za Marekani 300,000.

“Kwa mantiki hiyo, taarifa ya CAG inaonyesha Piper Links ilitozwa na kulipa kodi ya ongezeko la mtaji Sh 47,940,000 na Sh 4,800,000 kama ushuru wa stempu (stamp duty),” ilisema ripoti hiyo.

Katika mahojiano, Kamishna Mkuu wa TRA aliifahamisha kamati kuwa kwa gharama ya dola za Marekani milioni 20, kiasi cha kodi ya ongezeko la mtaji kilichotakiwa kulipwa ni Sh 6,399,977,600 na si Sh 47,988,800, na kwa upande wa ushuru wa stempu kiasi kilichotakiwa kulipwa ni Sh 320,000,000 na si Sh 4,800,000.

“Kwa maana hiyo, jumla ya kodi iliyopotea kwa maana ya kodi ya ongezeko la mtaji na ushuru wa stempu ni Sh 6,667,188,800.

“Jumla ya kodi iliyopotea kutokana na uuzaji wa hisa za Mechmar kwenda Piper Links na za Piper Links kwenda PAP ni Sh 8,683,177,600,” inasema taarifa ya PAC.

Ikulu, Bunge zarushiana mpira

Wakati hayo yakiendelea, Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, amesema chombo hicho hakiwezi kupeleka maazimio yake serikalini kwani Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambaye ndiye mtendaji mkuu wa shughuli za Serikali bungeni, alishayapokea na kuyatolea ufafanuzi siku ya kuahirisha Bunge.

Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku chache tangu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue kueleza kwamba ofisi yake haijapokea rasmi maazimio ya Bunge.

“Ninavyojua ni kwamba Bunge litaleta rasmi mapendekezo hayo serikalini,” alisema Balozi Sefue.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Dk. Kashililah alisema maazimio yalitolewa bungeni na kujibiwa na Waziri Mkuu, hivyo inamaanisha kwamba tayari yalishafika serikalini.

“Maazimio yalitolewa bungeni na baadaye Waziri Mkuu kuyatolea ufafanuzi, inamaanisha kuwa tayari yameshaifikia Serikali kwa kuwa yeye ndiye mtendaji mkuu wa Serikali bungeni,” alisema Dk. Kashililah.

Maazimio ya Bunge yameitaka mamlaka ya uteuzi kuwawajibisha wote waliotajwa kuhusika na kashfa ya Escrow.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles