30.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa: Kiongozi awe na ngozi kama ya tembo

Edward Lowassa
Waziri Mkuu wa zamani na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa

NA NORA DAMIAN, DAR ES SALAAM

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowasa amesema viongozi wenye maono na wasioogopa kusemwa ndio wanaotakiwa katika dunia ya sasa.

Lowasa aliyasema hayo jana alipokuwa akizindua helkopta ya Kanisa la Ufufuo na Uzima na vitabu tisa vilivyoandikwa na Askofu wa kanisa hilo, Josephat Gwajima.

“Hapa duniani kuna viongozi wa aina mbili, kuna viongozi ambao kazi yao ni kusimamia mahesabu na viongozi wenye maono.

“Na katika dunia hii ukitaka kushinda unatakiwa uwe na maono, mahusiano na mashirikiano mazuri na wenzako. Ukiogopa kusemwa hapa duniani hutaishi, unatakiwa kuwa na ngozi kama ya tembo,” alisema.

Kuhusu mgogoro wa ardhi unaolikabili kanisa hilo, Lowasa alisema atahangaika ili kuhakikisha kanisa hilo linafanikiwa kupata ardhi na kujenga kanisa kubwa.

Awali Askofu Gwajima alisema, amenunua helkopta hiyo kwa malengo mawili ambayo ni kusaidia watu wakati wa majanga mbalimbali pamoja na kueneza injili.

“Niliguswa sana wakati ilipotokea ajali ya kuzama kwa meli ya MV Spice, kama tungekuwa na helkopta ingesaidia kuokoa watu wengi zaidi ndio maana niliona ninunue itumike kwenye majanga na kueneza injili,” alisema Askofu Gwajima.

Alisema kuanzia Novemba 30 mwaka huu anatarajia kueneza injili kwa kutumia helkopta hiyo katika mikoa mbalimbali ikiwemo Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Rukwa, Katavi, Kigoma na Geita.

Mikoa mingine ni Kagera, Mwanza, Mara, Simiyu, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Lindi, Mtwara na katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Askofu huyo alisema mwakani anatarajia kununua helkopta nyingine tatu kwa ajili ya kusaidia kwenye majanga na kueneza injili.

Kuhusu vitabu hivyo alisema vina lengo la kumuongoza mtu kutoka kwenye matatizo.

Askofu huyo pia alimpongeza Lowasa kuwa ni miongoni mwa viongozi wachache wenye ujasiri na uthubutu wa kuamua.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa na maaskofu zaidi ya 10 kutoka makanisa mbalimbali nchini ambao kwa pamoja walimpongeza Askofu Gwajima kwa ununuzi wa helkopta hiyo kwani itasaidia kuufikia ulimwengu kwa haraka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles