30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

January ahofia kasi ya Rais Magufuli

January Makamba
January Makamba

Na Amina Omari, Tanga

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira),  January Makamba,  amehofia kasi ya utendaji kazi wa Rais Dk. John Magufuli na kuwaomba wazee wa Mkoa wa Tanga waendelee kumwombea dua.

Amesema dua za wazee hao ndizo zitakazomwezesha kufanya kazi inayokwenda sambamba na kasi ya kiongozi huyo mkuu wa nchi, ambaye amejipambanua kupinga ufisadi.

January ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli, alikuwa miongoni mwa wagombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), aliyefanikiwa kufika kwenye hatua ya tano bora katika mchakato huo.

Kauli hiyo aliitoa juzi wakati wa futari iliyoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigella, ambapo alisema  aliwaomba wazee wa mkoa huo waendelee kumwombea, ili aweze kufanyakazi vizuri kwani bado ana safari ndefu katika kazi zake za kisiasa.

“Kazi za kisiasa zina mambo mengi ili ufanikiwe ni lazima uombe baraka za wazee kama njia ya mafanikio ya safari hiyo.

“Bila dua zenu mambo hayawezi kwenda na kwa hakika ndiyo itakuwa taa yangu katika kutumia nafasi yangu ya uwaziri kulinga na kasi ya Rais wa awamu ya tano Dk. John Magufuli.

“Nadhani mnaiona kasi ya Rais wetu Dk. Magufuli aliyokuwa nayo na miye kijana wenu nipo kwenye majukumu ya kuhakikisha namsaidia katika utekelezaji wa majukumu hayo kupitia wizara yangu,” alisema January.

Alisema kazi ya siasa ni ngumu na ina changamoto nyingi katika utekelezaji wake  ikiwemo kuhitajika uvumilivu wa hali ya juu.

“Hii nafasi niliyokuwa nayo inahitaji umakini wa hali ya juu katika kupambana na majukumu ya maamuzi pamoja usimamizi wake hivyo niwaombe wazee wangu mnikumbuke katika sala zenu ili niweze kufanya vizuri,” alisema .

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine  Shigella aliwaomba viongozi wa dini mkoani humo kuuombea amani mkoa huo kutoka na kuibuka kwa vitendo vya uvunjifu wa amani ikiwemo mauaji  yaliyoibuka hivi karibuni.

Alisema kuwa licha ya kuwa Mkoa wa Tanga unasifika kwa uwepo wa amani na upendo lakini vitendo vya uvunjifu vimetoa picha mbaya.

“Tanga tulikuwa hakuna matukio ya uhalifu hadi kufikia kuchinjana lakini kwa matukio ya hivi karibuni yametoa taswira tofauti ya mkoa wetu hivyo niwaombe viongozi wa dini muombee amani ya mkoa irudi kama zamani,” alisema Shigella.

Pamoja na hali hiyo aliwataka viongozi hao wa dini kuhakikisha wanahamasisha amani na utulivu kwa waumini wao ili kuvutia uwekezaji mkubwa unaotarajiwa kuwepo katika mkoa huo wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles