26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Ni kizaazaa

mtz1NA WAANDISHI WETU, DODOMA/DAR

NI kizaazaa. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya migomo na fukuzafukuza ya wanafunzi kutawala katika vyuo vikuu nchini hali ambayo inaonekana kuibua hisia miongoni mwa Watanzania.

Kufuatia kurudishwa nyumbani kwa wanafunzi 7,802 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Jumuiya ya Wanataaluma wa chuo hicho, imevunja ukimya na kubaini mikakati yenye shaka dhidi ya uongozi.

Kutokana na hali hiyo wanataaluma hao wamelaani kitendo cha kurudishwa nyumbani kwa wanafunzi hao wa programu maalumu ya ualimu wa msingi na sekondari bila kupewa muda wa kutosha kujiandaa kwa kuzingatia umri wao na mazingira waliyokuwa wanaishi.

Tamko la jumuiya hiyo lilitolewa jana na kusambazwa kwa vyombo vya habari na katibu wake, Lameck Thomas, ambaye alisema lawama zimekuwa zikitupwa kwa walimu kutokana na taarifa hizo kutolewa na upande mmoja wa utawala pekee kwenda serikalini bila uwepo wa ushirishwaji wowote wa wahadhiri kupitia jumuiya yao.

Kutokana na hali hiyo, Thomas alisema si busara wao kama jumuiya kukaa kimya kwa jambo hilo bila kueleza usahihi wake kwa kina, hasa katika madai ya fedha ambapo kumekuwa na uchezewaji wa tarakimu.

“Si kweli kuwa walimu tuligoma kufundisha programu hii kama inavyoelezwa sehemu mbalimbali,” alisema Thomas.

Alisema tatizo kubwa ni kutokuelewana kati ya walimu na menejimenti ya chuo kutokana na mazingira mabovu ya uendeshaji wa programu hiyo chuoni hapo, ambapo malalamiko hayo waliyatoa tangu iliponzishwa.

“Na kumekuwa hakuna dalili yoyote ya ufumbuzi huku wakiendelea kufundisha kwa uzalendo mkubwa. Jumuiya ya Wanataaluma inapata hisia kuwa wizara imeamua kwa makusudi kushirikiana na uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma kupotosha uhalisia wa jambo hilo kwani hakuna hata wakati mmoja ambapo wamefanya mawasilianao na walimu kupata taarifa kutoka upande wao,” alisema.

Katibu huyo alisema kuwa katika kutafuta ufumbuzi kuhusu mgogoro huo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Stella Manyanya, alikutana na menejimenti ya chuo hicho Mei 19, mwaka huu chuoni hapo ambapo katika kikao hicho wajumbe walikubaliana kwa pamoja kuundwa kwa kamati ndogo ya kufuatilia suala hilo.

 

UTATA WA MADAI

Alisema madai yanayoelezwa na menejimenti si sahihi na taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, imepotosha kwani haijaeleza ukweli wa madai yaliyowasilishwa na chuo husika.

“Mfano katika Kitivo ‘Koleji’ cha Sayansi Asilia na Hesabu taarifa inasema yaliwasilishwa madai ya shilingi milioni 367.88 na kupungua mpaka shilingi milioni 90. Wakati uhalisia ni kwamba madai hayo hata kama yangebanwa kwa namna gani yasingepungua mpaka chini ya shilingi milioni 223.78,” alisema Thomas.

Alisema kuwa Kitivo cha Kompyuta taarifa inasemwa waliwasilisha madai yanayozidi sh milioni 100 wakati taarifa za Koleji zinasema madai halisi ni Sh milioni 53.7.

“Kwa nini utaratibu wa malipo uliotumika mwaka jana haukutumika wakati ulifanyika bila ya kuleta matatizo yanayoonekana wakati huu? Kama tatizo ni uhakiki wa madai kwa nini mpaka sasa tunapoongea walimu wa Koleji za Ualimu na Sayansi Asilia na Hesabu hawajalipwa hata senti moja ambapo ni katikati ya muhula huu wakati walifundisha muhula uliopita?’’ alihoji Thomas.

Katibu huyo alipinga kile alichodai kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, alitoa kauli ya upande mmoja Mei 30, mwaka huu suala ambalo haliwezi kuleta utatuzi wa kudumu kwani walimu hao wana mambo mengi ya kuzungumza ikiwamo mgogoro wa madai yao.

“Mfano mpaka sasa katika Koleji ya Sayansi Asilia na Hesabu kuna upungufu wa walimu 128 waliokuwa wanahitajika kufundidha programu hiyo kwa ufanisi, kwa muhula uliopita ni walimu 72 tu ndiyo waliobeba mzigo wa upungufu huo na kwa muhula huu hali ilikuwa inaelekea kuwa mbaya sana,” alisema.

Alisema kuwa wingi wa wanafunzi na uhaba wa walimu ulisababisha upangaji wa ratiba ya kufundisha kuwa ngumu kutokana na kozi kugawanywa katika mikondo mingi ambayo walimu walilazimika kuifundisha huku wakiwa na majukumu ya kufundisha kozi za shahada na majukumu mengine.

 

RAIS MAGUFULI

Akizungumza jana katika sherehe za utoaji tuzo za rais kwa wazalishaji bora viwandani kwa mwaka 2015, Rais Dk. John Magufuli alisema kuwa anashangazwa na wanasiasa wanaotetea watu waliopata daraja la nne kutaka waachwe wasome chuo kikuu.

“Ukigeuka hivi unakutana na wanafunzi hewa, ni nchi hii tu ambapo mtu unaweza kupata Divisheni 4 ya form 4 ukaingia chuoni na ukapata mkopo wa Serikali wakati wa form 6 hawapati mkopo. Ni nchi hii tu na anatoka mtu mwanasiasa mmoja anasema hawa wangesoma tu… kama tulifanya makosa ni lazima tuyamalize.

“Ninyi mnafahamu mtu ukimaliza form four (kidato cha nne) ukifeli sana sana utakwenda kuanzia certificate (cheti), ukifaulu then (halafu) unakwenda kuchukua diploma, baada ya miaka kadhaa tungejikuta ni Taifa la watu wa ajabu sana, ninasema haitawezekana, kama tuliyafanya makosa ni lazima tuyarekebishe na wakati ni sasa. Tuache siasa kwenye makosa,” alisema Rais Magufuli.

 

WANAFUNZI WAFUNGUKA

Baadhi ya wanafunzi waliorudishwa nyumbani katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), wameelezea kushangazwa na tangazo lililotolewa la kutakiwa kurudi nyumbani huku wakiwa hawana kosa lolote.

Mmoja wa wanafunzi hao aliyejitambulisha kwa jina la Praygod Emmanuel, alisema kuwa aliyekuwa chuoni hapo mwaka wa pili akichukua Diploma ya Sayansi ya Ualimu, alisema anashangaa wao kufukuzwa mithili ya wanyama huku kosa likiwa si la kwao.

“Tunashangazwa kufukuzwa mithili ya wanyama, sasa hivi tunaishi kwa hofu na hatujui hatma yetu kwani tunaambiwa tutaona katika vyombo vya habari na kwenye mtandao wa chuo,’’ alisema.

Naye Joshua Meshack alisema kwa sasa hawajui hatima yao na kuiomba Serikali kuwaangalia kwani hawana wanachotegemea zaidi ya elimu waliyokuwa wakiipata ili ije iwasaidie katika siku za usoni.

Meshack alisema kinachowaumiza zaidi ni kutofanya kosa lolote, lakini wamejikuta kwenye adhabu na mateso makubwa ikiwamo kukosa fedha za kuwawezesha kurudi makwao.

“Sisi hatuna kosa, kosa ni la watu wengine vipi tuumie sisi? Maisha yetu ni ya shida, mimi sijarudi nyumbani nipo na sina hata nauli ya na sijui nitafikaje nyumbani,” alisema.

 

PROFESA NDALICHAKO

Juzi jioni akitoa taarifa ya Serikali bungeni, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Ndalichako, aliahidi kupitia upya mfumo wa utoaji wa mafunzo ya stashahada maalumu kwa walimu wa sayansi Udom ili kuondoa matatizo yaliyopo.

Alisema Serikali imeamua kupitia mfumo huo ili kuufanyia marekebisho na kuweza kuwasaidia wanafunzi wa kada hiyo.

“Serikali itashirikina na uongozi wa chuo cha Udom kupitia upya mfumo wa utoaji wa mafunzo hayo ya diploma ya sayansi, tutaangalia utaratibu mzuri zaidi ambao utakuwa na tija kwa wanafunzi, wahadhiri na Taifa kwa ujumla,” alisema Profesa Ndalichako.

Aliongeza kuwa walimu wanaofundisha stashahada ya ualimu wa masomo ya sayansi walianza mgomo Mei 9, mwaka huu kutokana na madai ya malipo ya muda wa ziada wanaotumia kuwafundisha wanafunzi hao.

Alisema baada ya malalamiko uongozi wa chuo uliamua kuhakiki madai yao na yalipohakikiwa yalionekana yapo juu kwa mujibu wa sera ya chuo na uzito wa kazi, yaani walipaswa kulipwa posho hiyo.

Profesa Ndalichako alisema kuwa kiasi cha madai kilichowasilishwa ni Sh milioni 934 wakati fedha  zilizohakikiwa ni Sh milioni 252 kiasi ambacho waajiri wamekipinga.

 

UAMUZI WAPINGWA

Hata hivyo uamuzi huo wa Serikali kuwaondoa wanafunzi wa Udom chuoni uliotolewa bungeni na Profesa Ndalichako umepingwa kila kona na wadau mbalimbali wakiwamo walimu, wazazi wa watu wa kawaida.

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimemuomba Rais Magufuli kumaliza sakata hilo la wanafunzi bila kuendelea kuwaathiri.

Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk. Helen Kijo- Bisimba, alisema Dar es Salaam jana kuwa Rais Magufuli anapaswa kuliangalia kwa jicho la karibu tatizo la wanafunzi hao kwa sababu wananyanyasika na kudhalilishwa.

“Kimsingi mgogoro ulipofikia Rais Dk. Magufuli aone umuhimu wa kusuluhisha kwani kwa taarifa zilizopo wanafunzi hawa wanadhalilika, kunyanyasika wakati waliowapeleka chuoni hapo ni Serikali yenyewe,” alisema Dk. Helen ambaye pia ameutaka uongozi wa Bunge kuwarejesha wabunge wote waliosimamishwa waendelee na vikao ili kuwawakilisha wananchi wao.

Dk. Helen alisema kuwaondoa wanafunzi hao bila kuwapa nauli, kuwaandalia mazingira salama ni hatari kwa kuwa wengi wametoka kwenye familia masikini na hawakuja kimakosa katika chuo hicho bali ilikuwa mpango wa Serikali.

Alisema mgomo wa walimu wa kudai masilahi haukupaswa kuwaadhibu vijana hao na badala yake Serikali ichukue nafasi ya kuzungumza na walimu hao ili kumaliza tatizo hilo kwa njia ya amani.

“Inasikitisha watoto hao kufukuzwa chuoni, tena kwa kupewa saa 24 kama wahalifu wa makosa ya jinai wakati waliingia chuoni hapo kwa taratibu na vigezo vya Serikali kupitia Tume ya Vyuo Vikuu (TCU).

“Watoto hawa wametimuliwa kama wakimbizi au wahalifu kwa kupelekewa polisi wenye mabomu ya machozi bila kujali hali yao ya kiuchumi, kisaikolojia wala utu, huu ni ukiukwaji wa haki za binadamu uliofanywa ndani ya nchi ambayo inajinasibu kutekeleza demokrasia, sheria na haki za binadamu.

“Kwa maana hiyo kiongozi huyo haoni haja ya maisha ya wanafunzi hao hata kama wakibakwa, kutekwa, kuuawa kwani kwake hilo si jambo la dharura na halihitaji muda wa kujadiliwa,” alisema Dk. Helen.

 

WABUNGE KUTIMULIWA                      

Aidha Dk. Helen alizungumzia kusimamisha wabunge saba wa upinzani wasihudhurie vikao vya bunge vikiwamo vya bajeti.

Alisema miezi sita tangu bunge la 11 lianze  hakuna jipya ndani ya Bunge hilo mbali ya kushuhudia likiendeshwa kibabe na kisiasa.

“Katika kuonyesha ubabe wa kiti cha Spika wa Bunge hilo, tumeshuhudia wabunge saba wakipewa adhabu ya kutohudhuria vikao kwa vipindi tofauti kwa madai wamekidharau kiti katika kikao cha Januari 27, mwaka huu,” alisema.

Wabunge waliosimamishwa ni Tundu Lissu (Singida Mashariki), Esther Bulaya (Bunda Mjini), Pauline Gekul (Babati Mjini), Godbles Lema (Arusha Mjini), Halima Mdee (Kawe, John Heche (Tarime Vijijini) na Zitto Kabwe (Kigoma Mjini).

 

KAGERA

Mwenyekiti wa Chama Cha Walimu (CWT) Mkoa wa Kagera, Paul Kosta alisema uamuzi wa Serikali kuwarudisha nyumbani wanafunzi wa Udom kwa muda usiojulikana hauna nia njema kwa mustakabali wa elimu nchini.

Kosta ambaye pia ni mwalimu wa hisabati katika Shule ya Sekondari Rutabo iliyopo Tarafa ya Kamachumu wilayani Muleba, alisema lengo la Serikali kuweka utaratibu wa kusomea shahada kwa wanafunzi hao si wa bahati mbaya kwani ulitokana na nia yake ya kupunguza pengo la walimu wa sayansi linalolikabili taifa kwa sasa.

“Tumesikitishwa na hatua hiyo, mahitaji ya taifa kwa walimu wa sayansi bado ni makubwa kwa shule za msingi na sekondari, tunaambiwa Serikali ya sasa imevunja rekodi ya ukusanyaji kodi, kwanini inashindwa kuwalipa wahadhiri? alihoji.

Sunday Bubelwa ambaye ni mjasiriamali katika Mji mdogo wa Kamachumu alipiga simu MTANZANIA akisema hakuona sababu ya Naibu Spika kupinga hoja na Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari bungeni juzi.

“Vijana wetu tunasikia wamegeuka ombaomba na machangudoa katika mji wa Dodoma, Sisi tunajua mawaziri na baadhi ya wabunge wa CCM wanafanya hivyo kwa sababu watoto wao hawako katika mazingira kama hayo,” alisema Bubelwa.

 

DAR

Athman Mwamtemi ambaye ni dereva teksi katika Mtaa wa Samora jijini humo alisema: “Dk. Tulia amepotoka, hayo ni matumizi mabaya ya kiti kwa kukiuka haki ya msingi ya Bunge hilo kujadili suala zito kama hilo la elimu kwa watoto wa Tanzania.

“Ni haki ya wabunge kutetea masuala ya wananchi, hakuna sababu ya kuwafungia, haya ni matumizi mabaya ya kiti na hapa Naibu Spika amepotoka, anapaswa kukubali hilo na anapaswa kusahihisha makosa na kuacha ubabe,” alisema Chande.

 

WANAFUNZI UDSM WAGOMA

Wanafunzi wa shahada ya kwanza wanaonufaika na mkopo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), sehemu ya Mlimani, wameingia kwenye mgomo  kutokana na kucheleweshwa kwa fedha za kujikimu, huku wakimtaka RaisMagufuli kuwatumbua viongozi wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HELSB).

Pia wanafunzi hao wamekumbusha ahadi za Rais Magufuli wakati wa kampeni kuwa katika Serikali yake hatomvumilia  kiongozi wa bodi atakayechelewesha fedha za kujikimu za wanafunzi wa elimu ya juu.

Vuguvugu la mgomo huo lilianza juzi usiku katika hosteli za wanafunzi hao zilizopo Mabibo ambapo inadaiwa walikuwa wanapiga kelele za kudai fedha hizo wakilalamika kuwa wana njaa.

Akizungumza na MTANZANIA jana katika eneo linalotumika kwa mikutano ya wanachuo maarufu kama ‘Revolution Square’, mmoja wa wanafunzi ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini kwa kuhofia kufukuzwa chuo, alisema juzi walikutana na Rais wa Serikali ya Wanafunzi (DARUSO) ambaye aliahidi kuitisha mkutano wa wanafunzi wote kujua hatima ya malipo yao.

“Tumekusanyika hapa kutokana na agizo la rais wetu kuwa atakuja kuzungumza juu ya madai yetu ya kucheleweshewa fedha, jana (juzi) tulianza harakati hizo katika hosteli za Mabibo na leo (jana) hatujaingia darasani na hatutaingia hadi tupate fedha zetu,” alisema mwanafunzi huyo.

MTANZANIA ilifika katika eneo hilo jana saa 4 asubuhi na kushuhudia baadhi ya wanafunzi wakiwa wamekusanyika huku wengine wakipita kuelekea madarasani kuendelea na masomo kama kawaida.

Ilipofika saa 7 mchana rais wa DARUSO, Erasmi Leoni, aliwasili katika eneo hilo ambapo aliwataka wanafunzi hao kuwa na subira wakati akiendelea kuwabana utawala kutoa majibu huku akiwataka waendelee kubaki katika eneo hilo hadi watakapopata majibu ya kuridhisha.

“Naungana na ninyi kuendelea kukaa hapa hadi tutakapopata fedha zetu na tunatoa nusu saa kwa uongozi wa chuo kutupa majibu ya kupata fedha hizo leo (jana) na kama hawatatoa majibu ya kuridhisha tutachukua hatua zaidi,” alisema.

Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa Mikopo Tanzania ambaye pia ni Waziri wa Mikopo mstaafu wa UDSM, Evance Shitindi, alisema atashangaa kuona wanafunzi wanafukuzwa kwa mgomo huo badala ya kufukuzwa viongozi wa bodi huku akikumbushia ahadi ya rais kwa kuweka katika kipaza sauti, sauti iliyorekodiwa ya Rais Magufuli iliyokuwa katika simu yake.

Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Rwekaza Mkandala, aliliambia MTANZANIA kuwa chuo hakina mamlaka ya upatikanaji wa fedha hizo, lakini wanashirikiana na bodi kuhakikisha zinapatikana kwa wakati.

“Sisi kazi yetu ni kuhakiki majina ya wanafunzi wanaopokea mikopo ili kusiwepo hewa, lakini mpaka wakati huo waliwasiliana na bodi ya mikopo kwamba wamepeleka fedha hizo benki,” alisema Profesa Mkandala.

Mkurugenzi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo, Cosmas Mwaisoga, alisema mchakato wa malipo umekwishafanyika na hundi za malipo hayo zimepelekwa benki.

“Siku ya malipo ilikuwa ni Mei 28 mwaka huu ambayo ilikuwa Jumamosi na sisi siku hiyo hatufanyi kazi ndiyo maana sasa tunapigana kuharakisha mchakato ili wapate fedha zao haraka iwezekanavyo,” alisema.

 

CHUO CHA MAJI

Zaidi ya wanachuo 40 wanaosoma shahada ya uhandisi wa maji na umwagiliaji katika Chuo Kikuu cha Taasisi ya Maji (WDMI) nao wameandamana kwenda Bodi ya Mikopo wakilalamikia kucheleweshewa fedha za chakula na kujikimu.

Akizungumza na MTANZANIA kwa sharti la kutotajwa jina gazetini, mmoja wanachuo hao alisema wamefikia hatua hiyo baada ya bodi hiyo kushindwa kutoa fedha zilizotakiwa tangu Mei 20, mwaka huu.

Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa chuo hicho, Joseph Ikingu alisema taarifa waliyoipata kutoka kwa ofisa mikopo wa chuo hicho ni kwamba taratibu za kusaini hundi kwa ajili ya kutolewa fedha hizo zilikwishakamilika.

Meneja Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo nchini, Omega Ngole aliliambia MTANZANIA kuwa wanafunzi hao wanachokifanya ni upotoshaji kwani tarehe waliyopaswa kuanza kupokea mikopo yao ni Mei 26, mwaka huu hivyo hakukuwa na ucheleweshwaji.

Habari hii imeandaliwa na LEONARD MANG’OHA (MSJ), CHRISTINA GAULUHANGA NA FROLIAN MASINDE (DAR ES SALAAM), Ramadhan Hassan, Aziza Masoud (Dodoma)

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles