31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Jeshi la Magereza lamwaga ajira

Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja
Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja

NA PATRICIA KIMELEMETA, Dar es Salaam

JESHI la Magereza limetangaza nafasi mbalimbali za ajira katika jeshi hilo ambapo watakaochaguliwa watapatiwa mafunzo ya awali ya askari magereza yatakayoendeshwa na Chuo cha Magereza Kiwira, Tukuyu Mbeya.

Taarifa iliyotolewa jana na Kamishna wa jeshi hilo, John Minja, ilisema kuwa mwisho wa maombi hayo ni Oktoba 15 mwaka huu.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa watakaofanikiwa kuitwa katika usaili watajulishwa kupitia tovuti ya Jeshi la Magereza. www. magereza. go. tz, magazeti na katika mbao za matangazo ofisi za wakuu wa magereza wa mikoa na bwalo kuu la maofisa wa magereza lililopo Ukonga jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mwombaji anatakiwa kuwa raia wa Tanzania na kwamba awe na sifa mbalimbali ambazo ni pamoja na kutoajiriwa katika taasisi yoyote ya Serikali.

Sifa nyingine ni kwamba, asiwe ameoa au kuolewa na wala asiwe na mtoto. Mwombaji ambaye ni mhitimu wa shahada ya kwanza anatakiwa kuwa na umri wa kuanzia miaka 18 hadi 28 na wasiokuwa na shahada wawe na umri 18 na 24.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa, mwombaji mvulana awe na urefu usiopungua sentimeta 170.2 au futi 5 na inchi 7 na msichana awe na urefu usiopungua sentimeta 167.64 au futi  5 na inchi 4.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa, mwombaji ambaye amehitimu elimu yake kati ya mwaka 2012 hadi 2014 awe na afya nzuri iliyothibitishwa na daktari anayetambulika kisheria.

Taarifa hiyo ilizidi kufafanua kuwa, mwombaji awe hajawahi kushtakiwa au kupatikana na kosa lolote la jinai pia awe na tabia na mwenendo nzuri.

Ilibainisha kuwa awe na shahada katika fani au taaluma mbalimbali ambazo ni pamoja na shahada ya sheria, utekelezaji wa sheria, takwimu, uchumi na mipango, mazingira, usanifu majengo, ukadiriaji majengo, mipango na usimamizi wa miradi, uhandisi wa umeme, uhandisi wa mitambo ya kilimo na tiba ya mifugo.

Taaluma nyingine ni pamoja na misitu, uchumi, kilimo, bima, uhasibu na usimamizi wa vyama vya ushirika, uhandisi mazingira, sayansi na kompyuta, udaktari wa binadamu, ualimu wa masomo ya sayansi, kama fizikia, kemia, hisabati na baiolojia.

Ilibainisha kuwa mwombaji awe na taaluma ya ualimu wa masomo ya biashara na Kifaransa. Ukutubi, mahusiano, biashara na masoko.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mwombaji mwenye stashahada (Diploma) anatakiwa kuwa na cheti ambacho chuo chake kinatambulika na Serikali.

Mwombaji huyo anatakiwa kuwa na fani au taaluma mbalimbali ambazo ni pamoja na ukutubi, biashara na mipango, bima, uhasibu na usimamizi wa vyama vya ushirika.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa, taaluma nyingine ni pamoja na Mipango na Usimamizi wa Miradi, Utabibu, Uuguzi, Maabara na Mazoezi ya Viungo, Uhandishi wa Habari, Ufundi Magari, Ujenzi, Umwagiliaji, Mitambo ya Kilimo, Umeme, Usanifu Majengo, Ushauri Nasaha, Uhandisi Mitambo, Sanaa na Muziki, Ualimu wa Masomo ya Biashara, Uchumi na Kifaransa,

Mwombaji mwenye astashahada anatakiwa kuwa na fani mbalimbali ambazo ni pamoja na cheti cha majaribio ya ufundi katika fani za Uhandisi Maji, Ujenzi, Ufundi Magari, Umeme wa Magari, Waunganishaji Nondo.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa fani nyingine ni pamoja na Useremala, Bomba, Rangi, Ushonaji, Utengenezaji Sabuni, Ufumaji, Utengenezaji Viatu, Maabara, Muziki na Utamaduni, Uuguzi na Ukunga, Utabibu Msaidizi.

Taarifa hiyo iliwataka waombaji kuzingatia masharti yaliyotajwa ikiwa watabainika wamefanya udanganyifu wowote ikiwamo wa kutotimiza masharti yaliyotajwa hapo juu maombi yake yatatupwa.

Ilibainisha kuwa mwombaji ambaye atagundulika alifanya udanganyifu huo baada ya kupatiwa ajira, jeshi hilo litasitisha ajira yake, kuachishwa kazi na kufikishwa mahakamani.

Taarifa hiyo iliwataka waombaji kuwasilisha maombi yao moja kwa moja kwa Kamishna Jenerali wa Magereza, Makao Makuu ya Magereza kwa kutumia sanduku la posta 9190.

Ilieleza kuwa barua zote ziambatane na nakala zote za elimu, ujuzi, cheti cha kuzaliwa cha mwombaji pamoja na picha ndogo mbili za hivi karibuni.

Vyeti halisi vitatakiwa kuonyeshwa wakati wa usaili, hati ya mitihani haitapokelewa isipokuwa kwa wahitimu ambao vyeti vyao havijatoka katika vyuo husika pekee.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles