23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Kikwete kuwaleta Ronaldo, Messi

Rais Jakaya Kikwete
Rais Jakaya Kikwete

Na Abducado Emmanuel, Dar es Salaam

BAADA ya ujio wa magwiji wa zamani wa timu ya Real Madrid kufanyika kwa mafanikio makubwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, ameeleza kuwa anafanya uwezekano wa kuileta timu halisi ya Real Madrid yenye nyota, Cristiano Ronaldo au Barcelona yenye staa, Lionel Messi.

Magwiji hao walicheza mechi ya kirafiki dhidi ya magwiji wa zamani wa Tanzania ‘TSN Tanzania Eleven’, iliyoisha kwa Real Madrid kushinda kwa mabao 3-1, huku nyota wa mechi akiwa mshambuliaji, Ruben de la Red aliyefunga mabao matatu ‘hat trick’.

Rais Kikwete alieleza nia yake hiyo juzi usiku kwenye hafla ya kula chakula cha usiku na magwiji wa timu hizo, huku akisema tayari wameanza mazungumzo na Real Madrid, kufanikisha ujio wa timu hiyo halisi.

“Nimefarijika na ujio huu mkubwa nchini, ila kwa sasa nia yetu ni kuileta timu halisi yenyewe, tunafanya nao mazungumzo na timu hiyo hivi sasa ili kufanikisha hilo na hata magwiji hawa watatuunga mkono kwa hilo kutusaidia,” alisema akiwaambia wachezaji wa kikosi cha ‘TSN Tanzania Eleven’.

“Magwiji hawa waliotua nchini wametuambia ni rahisi Madrid kuja hapa, katika kipindi cha kujiandaa na msimu mpya wa ligi ‘pre season’ na sio nyakati kama hizi ambazo ipo kwenye mashindano,” alisema.

Kikwete alizidi kuongeza kuwa endapo nia ya kuileta Madrid itashindikana, basi watahamia pia kwa wapinzani wao Barcelona, kwa kuwatumia moja ya wadhamini wao Kampuni ya bia ya Castle Lager yenye maskani yake nchini Afrika Kusini, kwa kuwashawishi kuwaleta nchini.

“Unajua nia ya mdhamini ni kupata soko la matangazo, hivyo tutakapowatumia Castle ni rahisi sana kupeleka ushawishi wao na kuileta Barcelona nchini, kwani ni njia mojawapo ya kujitangaza,” alisema.

Katika hatua nyingine, wachezaji wa zamani wa Tanzania wakiongozwa na makocha wao, Boniface Mkwasa, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ na Fred Minziro walimshauri Kikwete kutumia fursa hiyo ya ujio huo, kuwapeleka wachezaji wetu vijana kwa ajili ya kupata mafunzo ya soka na kutanua wigo wa kucheza soka la kulipwa huko.

Ujio wa magwiji hao nchini umeratibiwa na Kampuni ya Tanzania Sisi ni Nyumbani (TSN), kwa kushirikiana na Rais Kikwete pamoja na kampuni nyingine kama vile Tropical Electronics, Vodacom Tanzania, Fast Jet, Hoteli ya Ladger Plaza, Binslum Tyres na ATN Petroleum.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles