30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Polisi, albino wapambana Dar

Kamishna Suleiman Kova
Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova

NA SHABANI MATUTU

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limetumia mabomu ya machozi kuwatawanya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), waliokuwa wakizuia gari la polisi lililokuwa limebeba mtuhumiwa wa kutishia kuua albino kwa maneno.

Tukio hilo lilitokea jijini Dar es Salaam jana, ambako albino hao walivamia gari hilo na kuwataka askari polisi wamshushe ndani ya gari mtuhumiwa huyo aliyetambulika kwa jina la Ombeni Michael, ili wafahamu alikokuwa akipelekwa.

Vurugu hizo zilianza katika Mahakama ya Mwanzo Buguruni, ambako albino hao walivamia wakati kesi dhidi ya mtuhumiwa huyo ikiendelea katika mahakama hiyo.

Baada ya kusikilizwa kwa kesi hiyo na dhamana kuwa wazi kwa mujibu wa sheria, watu hao wenye ulemavu waliamsha hasira ya kupinga kupewa dhamana kwa mtuhumiwa huyo.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Septemba 3, mwaka huu.

Mwekahazina wa Chama cha Albino Tanzania, Abdillah Omary, alilazimika kuandika barua mahakamani hapo kupinga hatua ya kupewa dhamana kwa mtuhumiwa huyo.

Pamoja na kuandika barua hiyo iliyopokewa na mahakama, ilibainika kuwa na upungufu wa kisheria na kutakiwa kuifanyia marekebisho.

Lakini ghafla mtuhumiwa huyo alipotolewa mahakamani na kuingizwa kwenye gari la polisi, alivamiwa na walalamikaji hao na kuanza kumshambulia.

Baada ya kuona walemavu hao wa ngozi wamewazidi nguvu, askari waliamua kuondoa gari na kuelekea katika kituo cha Buguruni, ambako waliomba msaada na baada ya muda waliwanya kwa mabomu ya machozi.

Akizungumzia kuhusu hilo, Mwenyekiti wa Chama cha Albino Wilaya ya Temeke, Kasim Kibwe, alisema suala la kuwalinda ni dhahiri Serikali imeshindwa, hivyo kuomba msaada kutoka nje ya nchi.

Alisema hatua hiyo itawasaidia kulindwa wakati wote, kwani matukio ya watu wenye ulemavu wa ngozi yamekuwa wakiongezeka kila siku.

“Inasikitisha kuona hapa nchini wanyamapori wanalindwa kwa nguvu kubwa kuliko sisi albino ambao ni binadamu, hali inayonifanya nifikirie kuwa mkimbizi nje ya nchi kuliko kuwa raia hapa nchini. Na hivi kuna uhusiano gani wa kuuawa kwa albino inapokaribia kipindi cha uchaguzi mkuu?” alisema Kibwe.

Kwa upande wake, Mwekahazina wa Chama cha Maalbino Taifa, Abdillah Omary, aliwataka albino wenzake kuwa watulivu katika kesi hiyo.

Kamanda wa Polisi Wilaya ya Ilala, Mary Nzuki, alithibitisha kutokea kwa vurugu hizo, huku akisema kuwa hali hiyo imechangiwa na mwili wa mwanamume mmoja aliyedhaniwa ni mlemavu wa ngozi kuokotwa amefariki dunia Tabata Kinyerezi mwishoni mwa wiki iliyopita.

Kamanda Nzuki alisema mwili huo kwa sasa upo katika uchunguzi unaowajumuisha viongozi wa Chama cha Albino Tanzania pamoja na wawakilishi wa Shirika la Under The Same Sun kubaini ukweli, na taarifa baada ya kukamilika zitatolewa wiki ijayo.

Alisema kuwa wakati wa tukio hilo, mmoja wa wananchi wa eneo hilo, Mwenyeusi Issa (39), alidai kumsikia mtuhumiwa, Ombeni Michael (34) akitoa kauli ya kutishia kuwaua albino, huku akiwa anakunywa pombe baa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles