31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Masheikh: Maaskofu msiingilie mchakato wa mahakama ya kadhi

DSC_0701Na Aziza Masoud, Dar es Salaam
TAASISI ya Masheikh na Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania, imepinga tamko la maaskofu kuhusu kuzuia kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi na kusema hatua hiyo ni sawa na kuingilia uhuru wa Bunge.
Kutokana na hali hiyo, wametaka maaskofu hao kupitia Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF), kuwaacha wabunge ili waweze kujadili muswada huo kwa uhuru bila kuwapo shinikizo katika suala hilo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa taasisi hiyo, Sheikh Khamis Mataka, alisema tamko lililotolewa na maaskofu ni sawa na kuingilia madaraka ya Bunge na kutaka kuifanya Serikali ichukiwe kwa kuonekana imeshindwa kutimiza ahadi iliyoitoa kupitia Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
“Tamko lililotolewa na maaskofu halina hoja, hawana sababu za msingi za kuikataa Mahakama ya Kadhi, tunawasihi na kuwaomba maaskofu waachie uhuru wa wabunge hasa waumini wa dini ya Kikristo walioko bungeni, ili waweze kuujadili muswada huo bila shinikizo la kiimani.
“Mbinu zozote za kuwashawishi wabunge kiimani kutekeleza maazimio ya maaskofu chini ya Jukwaa la Wakristo Tanzania zitaleta udini na jaribio la kuligawa Bunge kiimani, jambo ambalo ni hatari kwa mustakabali wa taifa letu,” alisema Sheikh Mataka.
Alisema wabunge wanapaswa kuzingatia viapo vyao vya kuwatumikia wananchi kwa uadilifu bila kuathiriwa na shinikizo la kiimani lililotolewa na maaskofu.
Sheikh Mataka alisema taasisi inawakumbusha maaskofu kwamba Serikali ina vyombo vya uchunguzi na utafiti vyenye uwezo wa kubaini maeneo yanayovunja umoja wa kitaifa pamoja na mambo yanayokwenda kinyume na Katiba ya nchi ambapo wao si sehemu ya vyombo hivyo.
Alisema hofu ya kuwapo kwa Mahakama ya Kadhi bara ni bandia kwa kuwa kesi za Kiislamu zinazohusu masuala ya talaka, mirathi, wosia, wakfu na malezi ya watoto zinaamuliwa kwa sheria na taratibu za dini hiyo.
“Wanachoomba Waislamu ni kubadilishwa hakimu na kuondoa malalamiko na uonevu, hasa kwa wanawake ambapo lengo ni kuwapo mtu anayejua sheria na kuamua kuamua kesi hizo,” alisema.
Sheikh Mataka, ambaye pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya Bakwata Taifa, alisema migogoro ya kiimani ya ndani, hasa kwa Waislamu isitumike kama kigezo cha kupinga mahakama hiyo kwa upande wa Tanzania Bara.
Alisema Mahakama ya Kadhi haihusiani na migogoro ya Wakristo, bali ni kuamua masuala ya Waislamu, huku akishangazwa na hatua ya maaskofu hao kupinga mchakato huo hali ya kuwa hauwahusu na wala haugusi imani yao.
“Tutashangaa iwapo Serikali itaamua kuuondoa bungeni muswada unaolenga kuitambua Mahakama ya Kadhi kwa kuitungia sheria maalumu. Je, iweje leo kuwa na maneno ya kila aina ya kushinikiza kuondolewa kwa muswada huo, hili hapana, wabunge waachwe waamue kwa utashi wao na sio kuingiliwa na makundi ya nje,” alisema.
Sheikh Mataka alisema kama Mahakama ya Kadhi ingekuwa na matatizo, ni wazi isingeanzishwa kwa upande wa Zanzibar ambako hadi sasa imekuwa ikitumika pasi na kuwapo na migogoro ya aina yoyote.
Juzi, viongozi wengine wa dini ya Kiislamu walipinga tamko lililotolewa na Jukwaa la Wakristo kuhusu sheria hiyo ya kuanzishwa Mahakama ya Kadhi na kudai kuwa matamko ya aina hiyo yanaweza kusababisha machafuko nchini.
Kauli hiyo zimekuja baada ya Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) kutoa waraka juzi, likipinga muswada unaopendekeza kuanzishwa Mahakama ya Kadhi unaotarajiwa kuwasilishwa bungeni wakati wowote.
Kutokana na hali hiyo Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju, aliwatoa hofu Wakristo wanaohofia mpango wa Serikali wa kuitambua kisheria Mahakama ya Kadhi nchini.
Alisema pamoja na kwamba mpango huo umeanza kulalamikiwa na baadhi ya makundi ya kidini, nia hiyo haina madhara kwa wananchi kwa kuwa Serikali haiwezi kupitisha sheria itakayowagawa watu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles