25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yatoa uhakika wa soko la dawa nchini

Sidi Mgumia-Aliyekuwa Kibaha

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Ustawi  wa Jamii, Jinsia, Wazee  na Watoto, imetoa uhakika wa soko kwa wawekezaji wanaojenga viwanda vya dawa nchini.

Mbali ya kuwahakikishia wawekezaji hao soko, lakini pia imeahidi kuzinunua dawa hizo kwa bei itakayokuwa na tija kwa wamiliki wa viwanda hivyo.

Uhakika huo umetolewa hivi karibuni na Waziri wa Wizara hiyo, Ummy Mwalimu, alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa viwanda viwili vya dawa unaoendelea Kibaha, mkoani Pwani.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukamilisha ukaguzi wa ujenzi wa viwanda hivyo vya Kairuki Pharmaceutical Industrial Limited (KPIL) na Vista Pharma Limited vilivyopo eneo la Zegereni wilayani hapa, Waziri Ummy alisema lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha dawa, vifaa na vifaa tiba vinapatikana kwa urahisi kwenye kila hospitali nchini.

Amesema serikali imetoa kipaumbele kwenye viwanda vya ndani vya dawa kwa nia ya kukabiliana na changamoto nne zinalolikabili eneo hilo.

Miongoni mwa changamoto hizo ni kutumia fedha nyingi nje ya nchi kwa ajili ya kununua dawa, ambapo katika kila Sh 100, Sh 94 zinakwenda nje ya nchi.

Alisema kwa sasa Tanzania ina takribani viwanda 11 vya dawa, lakini bado uzalishaji wao si mkubwa unaoweza kuhimili mahitaji ya soko la ndani.

Alisema pia ipo changamoto ya muda wa kupata dawa, inachukua muda mrefu kufika nchini kutokana na mlolongo wa taratibu za kuagiza na ndiyo maana serikali imeona haja ya kuwekeza nguvu kubwa kwa wawekezaji walioamua kujenga viwanda vya dawa nchini.

“Changamoto tunayopitia Serikali mbali na kwamba tunatumia fedha nyingi katika uagizaji wa dawa, bado dawa hizi zinachelewa kufika, Bohari ya Dawa (MSD) imekuwa ikiagiza dawa nje ya nchi na dawa hizo hukaa takribani zaidi ya miezi sita ndio zinaingia nchini, jambo hili hufanya upatikanaji wa dawa usiwe rahisi.

 “Kati ya wadau 72 wa masuala ya afya nchini walioomba kujenga viwanda vya dawa hapa nchini, ni nane mpaka sasa ndio wameanza kujenga na kati ya hao, sita viwanda vipo Kibaha,” alisema.

Kuhusu tozo, Waziri Ummy alisema tayari serikali imeshafuta baadhi ya tozo na kama zipo zinazowakwaza yuko tayari kukaa chini na wadau na kuona namna ya kuziondoa.

Na hayuko tayari kuona kuna ukwamishaji wa aina yoyote unafanyika katika kufanikisha ndoto ya Tanzania ya viwanda na alimtaka Mkuu wa Wilaya kuhakikisha anasimamia hilo.

Kwa upande wa soko, Waziri Ummy alisema serikali kwa sasa inanunua dawa zinazozalishwa ndani kwa bei kubwa kuliko zile zinazozalishwa nje.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles